Showing posts with label vitabu pepe. Show all posts
Showing posts with label vitabu pepe. Show all posts

Thursday, May 18, 2017

Vitabu Nilivyonunua Jana

Jana nilinunua vitabu vitatu katika duka la vitabu la chuoni St. Olaf. Viwili, Two Years Eight Months and Twenty-Eight Nights cha Salman Rushdie na A Strangeness in my Mind cha Orhan Pamuk, niliviona juzi. Cha tatu, Why Homer Matters, kilichotungwa na Adam Nicolson, nilikiona hiyo hiyo jana.

Nilipoingia dukani, nilikumbuka makala niliyoisoma juzi usiku, kuhusu vitabu halisi na vitabu pepe. Makala hii, sawa na nyingine nyingi, inatafakari iwapo vitabu vya jadi vitasalimika katika himaya hii ya vitabu pepe. Lakini inahitimisha kuwa hakuna ushahidi kuwa vitabu vya jadi vitapoteza mvuto au kufifia.

Mimi ni mmoja wa wale ambao hatujabadilika. Bado tumezoea vitabu halisi, yaani vitabu vya jadi, na ndio maana sisiti kuvinunua, wala sisiti kuelezea tabia yangu hiyo. Hapa nitaelezea kifupi kwa nini nimenunua vitabu hivi vitatu.

Kitabu cha Salman Rushdie kilinivutia kwa sababu ya umaarufu wa mwandishi huyu. Bila shaka wengi watakumbuka kitabu chake, Satanic Verses, ambacho kilipigwa marufuku katika nchi nyingi kwa madai kuwa kinaukashifu u-Islam. Ayatollah Khomeini wa Iran alitangaza fatwa kuwa Salman Rushdie anapaswa kuuawa.

Duniani kote, na hata miongoni mwa wa-Islam wenyewe hukumu hii ilizua mjadala. Baadhi walisema kuwa fatwa haikupaswa kutolewa kabla ya Salman Rushdie kupewa fursa ya kujieleza na kukiri kosa lake. Watu wengine walisema kuwa zogo hili lilimpa Salman Rushdie umaarufu ambao hakustahili kwa kigezo cha ubora wa uandishi wake.

Ninavyo baadhi vitabu vya Salman Rushdie, kikiwemo hiki cha Satanic Verses. Nimemewahi kufundisha riwaya yake maarufu, Midnight's Children. Ninavutiwa na ubunifu wake katika kuelezea mambo, na uhodari wake wa kutumia lugha. Uandishi wake unasisimua na kufikirisha.

Orhan Pamuk ni mwandishi ambaye nimewahi kumtaja katika blogu hii. Nina vitabu vyake kadhaa, na nimekuwa na hamu ya kuvisoma, ila bado sijapata wasaa. Huyu amenivutia si tu kwa kuwa alipata tuzo ya Nobel, bali pia kwa sababu ninafahamu kiasi fulani kuhusu fasihi simulizi ya Uturuki, kama vile hadithi za Nasreddin Hodja na Dede Korkut.

Why Homer Matters nimekipenda kwa kuwa taaluma ya tendi nimeipenda na kuishughulikia kwa miaka mingi. Homer, ingawa taarifa zake hazijulikani vizuri, ndiye anayehusishwa na tendi maarufu za u-Griki ya kale, The Iliad na The Odyssey. Kwa kuangalia juu juu, niliona kuwa mwandishi wa Why Homer Matters ana uwezo mkubwa wa kuelezea masuala ya Homer na hizi tendi.

Thursday, December 29, 2016

Vitabu Tulivyosoma Mwaka 2016

Zikiwa zimebaki siku mbili tu kabla ya kwisha mwaka 2016, nimeona wa-Tanzania kadhaa wakijitokeza katika mtandao wa Facebook na kutaja vitabu walivyosoma mwaka huu. Jambo hili limenifurahisha, nikizingatia kuwa nimekuwa nikihamasisha usomaji wa vitabu, kwa kutumia blogu yangu hii, blogu za wengine, na pia katika kitabu changu, CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Ninawapongeza watu hao kwa kuonyesha mfano mzuri. Ninawapongeza pia wasomaji waliojitokeza na kuchangia suala hili kwa namna mbali mbali, kama vile kuvijadili vitabu hivyo, kuulizia upatikanaji wake, au kupendekeza vitabu vingine. Kuhusu upatikanaji wa vitabu, watu wamepeana taarifa za maduka ya vitabu, na pia upatikanaji wa vitabu pepe mtandaoni. Ni jambo la kuvutia kwamba kuna wa-Tanzania wanaotambua matumizi ya manufaa ya tekinolojia ya mtandao.

Mazungumzo haya yameonyesha mambo kadhaa. Jambo moja ni kuwa wako wa-Tanzania wanaojibidisha kusoma vitabu. Jambo jingine ni kuwa wanasoma vitabu vya aina mbali mbali, kama vile vya siasa, ujasiriamali, fasihi, na maendeleo ya jamii au ya mtu binafsi. Vile vile wanasoma vitabu vya waandishi wa mataifa mbali mbali, vya ki-Swahili na vya ki-Ingereza. Jambo jingine ni kuwa wahusika wameonyesha moyo mkubwa wa kusaidiana, kama vile kwa kufahamishana vitabu bora na hata kuazimishana vitabu.

Ninawaenzi watu hao. Huenda wakawa chachu ya kustawisha utamaduni wa kusoma vitabu nchini Tanzania. Laiti watu wengi zaidi wangejumuika katika safari hii. Laiti kama watu maarufu nchini mwetu, kama vile wanasiasa na wasanii, wangejiunga na kuwa wahamasishaji wa usomaji wa vitabu. Kutokana na mvuto wa wasanii wetu, kwa mfano, wangeweza kuwa wahamasishaji wa watoto na vijana katika kupenda kusoma vitabu.

Kwa upande wangu, naona sihitaji kuorodhesha vitabu nilivyosoma mwaka 2016. Mara kwa mara, katika blogu hii au blogu ya ki-Ingereza, ninaandika taarifa za baadhi ya vitabu ninavyosoma. Vingine ni vile ninavyofundisha chuoni St. Olaf, na vingine ni vile ninavyojisomea mwenyewe. Ninapoandika  taarifa, ninajitahidi kuelezea upekee au ubora wa vitabu hivyo.

Saturday, December 19, 2015

Kuchapisha Vitabu Mtandaoni

Kutokana na taarifa ninazoandika katika blogu hii, na sehemu zingine, watu wengi wanafahamu kuwa nimechapisha vitabu vyangu mtandaoni. Nimeshawasaidia waandishi kadhaa wa mataifa mbali mbali kuchapisha vitabu vyao kwa mtindo huo. Kwa upande wa Tanzania, niliwahi kuongea na wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuhusu suala hilo, na nilinukuliwa katika gazeti la Mwananchi.

Mara kwa mara, watu huniulizia kuhusu kuchapisha vitabu vyao. Napenda kuongelea tena suala hili, hasa matokeo ya kuchapisha vitabu mtandaoni. Kwanza, ni muhimu kufahamu kwamba kuna njia nyingi za kuchapisha vitabu mtandaoni. Ni juu ya mwandishi kuchagua. Binafsi, ninatumia njia ambayo ni rahisi kabisa, isiyo na gharama, au yenye gharama ndogo kiasi kwamba haiwi kizuizi kwangu.

Kuchapisha kwa namna hii ni rahisi sana. Mbali ya kutokuwa na gharama, haichukui muda, ili mradi mswada umeshaandaliwa kama faili la kielektroniki. Kinachobaki ni kuuingiza mswada kwenye tovuti ya kuchapishia, na haichukui dakika kumi kumaliza shughuli hii na kitabu kikawa tayari kununuliwa na watu popote ulimwenguni.

Jambo moja linalovutia sana katika kuchapisha vitabu mtandaoni kwa namna nifanyavyo ni kwamba vitabu hupatikana bila kikomo. Vinahifadhiwa kama mafaili ya kielektroniki, na huchapishwa kama kitabu halisi pale tu mdau anapoagiza nakala. Akiagiza nakala moja, inachapishwa hiyo hiyo. Akiagiza mia au elfu ni hivyo hivyo. Hakuna udhia wa kutunza shehena ya vitabu ghalani na kungojea wateja, huku vikiwa katika hatari ya kuharibiwa na unyevu, mende, au panya.

Hata hivi, nimeona kuna matatizo. Kwanza kwa upande wa mnunuzi. Ni lazima awe na namna ya kununua mtandaoni. Kwa kawaida hii inamaanisha awe na "credit card" kama vile VISA na Mastercard. Jambo la pili ni bei. Nikiangalia vitabu vyangu, naona wazi kuwa kama vingechapishwa mahali kama Tanzania kwa mtindo wa jadi, vingekuwa na bei nafuu kuliko ilivyo sasa.

Lakini, kwa upande mwingine, kama kitabu kinachapishwa kama kitabu pepe, yaani "e-book," kinaweza kuuzwa kwa bei ndogo sana, kuliko bei ya kuchapisha kwa mtindo wa jadi. Mdau anatakiwa awe na kifaa cha kuhifadhia na kusomea kitabu pepe, yaani "e-reader" au "e-book reader," kama vile Kindle au Nook.

Pamoja na kuwepo kwa vitabu pepe na vifaa vya kuhifadhia na kusomea vitabu hivyo, imethibitika tena na tena kwamba wadau wengi bado wanavitaka vitabu vya jadi, yaani vya karatasi na majalada. Mazoea haya na mapenzi ya vitabu vya jadi yamejengeka na hayaonekani kutoweka mioyoni mwa wengi.

Tekinolojia ya kuchapisha vitabu mtandaoni inawaathiri wachapishaji wa jadi kwa namna mbali mbali. Kadiri siku zinavyopita, wengi wao wanaona faida ya kuchapisha vitabu mtandaoni. Tekinolojia hii mpya inawasukuma kwenda na wakati ili wasipoteze biashara katika mazingira ya ushindani na mabadiliko yasiyoisha.

Saturday, February 28, 2015

Kitabu Kinapoingia Amazon

Kati ya majina yanayojulikana sana mtandaoni ni Amazon, duka la mtandaoni ambamo vinapatikana vitu mbili mbali. Wengi wetu, kama sio wote, tunalihusisha jina la Amazon na vitabu.

Wanunuaji wa vitabu mtandaoni moja kwa moja huwazia duka la Amazon. Mimi mwenyewe, katika matamasha ya vitabu ninayoshiriki, nimezoea kuulizwa na watu iwapo vitabu yangu vinapatikana Amazon. Hao ni watu ambao wangependa kununua vitabu vyangu ila hawana hela wakati huo. Waandishi wanaitegemea Amazon kama sehemu ya kuuza vitabu kwa urahisi, hasa ikizingatiwa kwamba Amazon imejijenga sehemu nyingi za dunia.

Binafsi, sikutaka kuviweka vitabu vyangu Amazon. Sikupendezwa na jinsi kampuni hii kubwa inavyowaharibia biashara wauzaji wadogo wadogo, kama yanavyofanya makampuni makubwa katika mfumo wa ubepari.

Nilitaka vitabu vyangu viuzwe na maduka madogo madogo, ya watu wa kawaida au taasisi za kawaida. Niliridhika kuona vitabu yangu vinauzwa na duka la vitabu la Chuo cha St. Olaf, kwa mfano.

Lakini, nilikuja kushangaa baadaye kuwa, ingawa sikuvipeleka vitabu yangu Amazon, vilianza kuonekana kule. Hapo nilitambua kuwa Amazon ina nguvu au mvuto kuliko nilivyodhania. Ni kama kifaru anayetembea nyikani bila kubughudhiwa na wanyama wadogo wadogo.

Amazon inauza vitabu vipya na pia nakala zilizotumika. Mtu akishanunua na kusoma nakala yake, anaweza kuiuza Amazon. Ukiangalia tovuti ya Amazon, utaona vitabu vyangu vipya vinauzwa sambamba na vilivyotumika.

Kutokana na hali halisi ya ushindani katika uchumi wa kibepari, Amazon inauza au inaweza kuuza vitabu kwa bei ya chini kidogo au sana, ukifananisha na wauzaji wengine, kuanzia wachapishaji hadi hasa wauzaji wadogo wadogo. Vile vile, malipo ("royalties") anayopata mwandishi kutokana na mauzo ya vitabu vyake Amazon huwa ni pungufu kuliko yale ayapatayo au anayoweza kuyapata kutoka kwa wachapishaji, ingawa nayo si makubwa, bali ni asilimia ndogo ya bei ya kitabu.

Pamoja na yote hayo, Amazon imetamalaki katika uwanja huu wa uuzaji wa vitabu mtandaoni. Ingawa kuna makampuni mengine pia, kama vile Barnes and Noble, Amazon ndio inayoonekana kutawala vichwani mwa watu.

Amazon inauza vitabu halisi, yaani vya karatasi, na vitabu pepe. Ni juu ya mwandishi kuamua kama anataka kukiweka kitabu chake katika mtindo wa kielektroniki. Inavyoonekana, kadiri siku zinavyopita, watu wengi zaidi na zaidi wanaingia katika mkondo huu wa kununua vitabu pepe. Mimi mwenyewe nimeshuhudia hayo, na nimekuwa nikijitahidi kwenda na wakati. Baadhi ya vitabu vyangu vinapatikana kama vitabu pepe kwenye mtandao wa lulu na mtandao wa Amazon.

Hata hivi, kuna mjadala mkubwa unaoendelea kuhusu hatima ya vitabu tulivyovizoea, yaani vya karatasi. Wakati wengine wanaamini kuwa vitabu hivi vitadidimizwa na vitabu pepe, wengine wanasema kuwa hilo halitawezekana, kutokana na mazoea na mapenzi yaliyojengeka kwa vitabu kama vitabu. Wanasema kuwa hivi vitabu vya jadi vitakuwepo sambamba na hivi vya kielektroniki.

Nimeona niseme hayo, kwa manufaa ya wengine ambao ni waandishi au wanawazia kuwa waandishi.

Saturday, October 6, 2012

Nimejipatia iPad

Pamoja na kuwa mimi ni mmoja wa wale watu wa zamani tuliozaliwa na kukulia kijijini na ambao tunababaishwa na hizi tekinolojia zinazofumuka kwa kasi, nimejipatia kifaa kiitwacho iPad siku chache zilizopita. Nimenunua iPad Wi-Fi+3G. Nilishinikizwa na binti yangu Zawadi. Ndiye anayenisukuma niende na wakati.

Tangu ninunue kifaa hiki, yapata wiki mbili zilizopita, nimekuwa katika kujifunza namna ya kukitumia, maana kina mambo mengi sana. Angalau naweza kutembelea mitandao, kutuma na kupokea barua pepe, na kupiga picha na kisha kuziangalia. Hata video najua namna ya kupiga.

Kitu ninachotaka kukifanya hima ni kuingiza vitabu pepe kwenye hii iPad, nikianzia na kitabu changu kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho wadau wanakipata mtandaoni, pamoja na vitabu vyangu vingine, kwa njia hiyo.





Kidogo najisikia vibaya kwamba nilikiweka kitabu hiki katika muundo wa kitabu pepe na wadau wanakinunua, wakati mimi mwenyewe sikuwa na kifaa cha kuingizia vitabu pepe wala sikuwahi hata kuona kinakuwaje katika umbo la kitabu pepe. Nimejisikia kama mpishi ambaye anawapikia wengine lakini yeye mwenyewe hata kuonja haonji. Sasa, na hii iPad yangu, ngoja nikae mkao wa kula, kwa vitabu vyangu na vya wengine.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...