Showing posts with label vitabu mtandaoni. Show all posts
Showing posts with label vitabu mtandaoni. Show all posts

Monday, March 2, 2015

Nimeulizwa Inakuwaje Siuzi Vitabu Vyangu Tanzania

Leo katika mtandao wa Facebook kuna mdau kaniuliza inakuwaje siuzi vitabu vyangu Tanzania. Nimemshukuru kwa ulizo lake, nikajaribu kulijibu. Napenda kuandika machache kuhusu suali hili.

Napenda kuanza kwa kusema kuwa vitabu hivyo vinapatikana mtandaoni, kama vile kwenye tovuti ya lulu na tovuti ya Amazon. Yeyote mwenye kadi ya "credit" kama vile VISA au MasterCard, anaweza kuvinunua. Haijalishi kama yuko Chake Chake, Dar es Salaam au Tukuyu. Ataletewa. Kama ana kifaa kama "kindle," ananunua bila tatizo.

Ninafahamu kuwa ni wa-Tanzania wachache walioko Tanzania wanaoweza kununua vitu mtandaoni. Lakini kuna maelfu ya wa-Tanzania katika nchi kama Marekani wenye hizo kadi. Kama kuna nia ya dhati ya kununua kitabu, haikosekani njia.

Mimi mwenyewe nimekuwa tayari kufanya mipango na wa-Tanzania wenye nia ya kuuza vitabu vyangu, kwa kuwapelekea. Nimewahi kufanya hivyo na Cultural Tourism Program (Longido), Bougainvillea Lodge (Karatu), na Cultural Tourism Program (Mto wa Mbu).

Kila inapowezekana, nafanya mpango wa kuvifikisha vitabu vyangu kwenye matamasha nchini Tanzania, kama ilivyoelezwa hapa.

Kwa kuwa mimi si mfanyabiashara, ningependa kuona wafanyabiashara wanajipatia faida kutokana vitabu vyangu. Duka la vitabu chuoni St. Olaf linauza vitabu vyangu kwa bei kubwa kuliko mtandaoni. Vile vile, nilipotembelea chuo cha South Central, katika duka la vitabu walikuwa wanauza kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kwa dola 17.95.

Hata hivi, huwa najiuliza ni wa-Tanzania wepi wanaotaka kusoma vitabu vyangu. Sijaona kama kuna utamaduni wa kununua na kusoma vitabu. Wa-Marekani ndio wasomaji wangu wakuu, kama ninavyobainisha mara kwa mara katika blogu hii. Kwa vyovyote, kuepusha lawama, na kuwatendea haki wa-Tanzania wanaoamini nina jambo la kuwaambia, najitahidi kuhakikisha vitabu vyangu vinapatikana Tanzania.

Saturday, February 28, 2015

Kitabu Kinapoingia Amazon

Kati ya majina yanayojulikana sana mtandaoni ni Amazon, duka la mtandaoni ambamo vinapatikana vitu mbili mbali. Wengi wetu, kama sio wote, tunalihusisha jina la Amazon na vitabu.

Wanunuaji wa vitabu mtandaoni moja kwa moja huwazia duka la Amazon. Mimi mwenyewe, katika matamasha ya vitabu ninayoshiriki, nimezoea kuulizwa na watu iwapo vitabu yangu vinapatikana Amazon. Hao ni watu ambao wangependa kununua vitabu vyangu ila hawana hela wakati huo. Waandishi wanaitegemea Amazon kama sehemu ya kuuza vitabu kwa urahisi, hasa ikizingatiwa kwamba Amazon imejijenga sehemu nyingi za dunia.

Binafsi, sikutaka kuviweka vitabu vyangu Amazon. Sikupendezwa na jinsi kampuni hii kubwa inavyowaharibia biashara wauzaji wadogo wadogo, kama yanavyofanya makampuni makubwa katika mfumo wa ubepari.

Nilitaka vitabu vyangu viuzwe na maduka madogo madogo, ya watu wa kawaida au taasisi za kawaida. Niliridhika kuona vitabu yangu vinauzwa na duka la vitabu la Chuo cha St. Olaf, kwa mfano.

Lakini, nilikuja kushangaa baadaye kuwa, ingawa sikuvipeleka vitabu yangu Amazon, vilianza kuonekana kule. Hapo nilitambua kuwa Amazon ina nguvu au mvuto kuliko nilivyodhania. Ni kama kifaru anayetembea nyikani bila kubughudhiwa na wanyama wadogo wadogo.

Amazon inauza vitabu vipya na pia nakala zilizotumika. Mtu akishanunua na kusoma nakala yake, anaweza kuiuza Amazon. Ukiangalia tovuti ya Amazon, utaona vitabu vyangu vipya vinauzwa sambamba na vilivyotumika.

Kutokana na hali halisi ya ushindani katika uchumi wa kibepari, Amazon inauza au inaweza kuuza vitabu kwa bei ya chini kidogo au sana, ukifananisha na wauzaji wengine, kuanzia wachapishaji hadi hasa wauzaji wadogo wadogo. Vile vile, malipo ("royalties") anayopata mwandishi kutokana na mauzo ya vitabu vyake Amazon huwa ni pungufu kuliko yale ayapatayo au anayoweza kuyapata kutoka kwa wachapishaji, ingawa nayo si makubwa, bali ni asilimia ndogo ya bei ya kitabu.

Pamoja na yote hayo, Amazon imetamalaki katika uwanja huu wa uuzaji wa vitabu mtandaoni. Ingawa kuna makampuni mengine pia, kama vile Barnes and Noble, Amazon ndio inayoonekana kutawala vichwani mwa watu.

Amazon inauza vitabu halisi, yaani vya karatasi, na vitabu pepe. Ni juu ya mwandishi kuamua kama anataka kukiweka kitabu chake katika mtindo wa kielektroniki. Inavyoonekana, kadiri siku zinavyopita, watu wengi zaidi na zaidi wanaingia katika mkondo huu wa kununua vitabu pepe. Mimi mwenyewe nimeshuhudia hayo, na nimekuwa nikijitahidi kwenda na wakati. Baadhi ya vitabu vyangu vinapatikana kama vitabu pepe kwenye mtandao wa lulu na mtandao wa Amazon.

Hata hivi, kuna mjadala mkubwa unaoendelea kuhusu hatima ya vitabu tulivyovizoea, yaani vya karatasi. Wakati wengine wanaamini kuwa vitabu hivi vitadidimizwa na vitabu pepe, wengine wanasema kuwa hilo halitawezekana, kutokana na mazoea na mapenzi yaliyojengeka kwa vitabu kama vitabu. Wanasema kuwa hivi vitabu vya jadi vitakuwepo sambamba na hivi vya kielektroniki.

Nimeona niseme hayo, kwa manufaa ya wengine ambao ni waandishi au wanawazia kuwa waandishi.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...