Showing posts with label Midnight's Children. Show all posts
Showing posts with label Midnight's Children. Show all posts

Thursday, May 18, 2017

Vitabu Nilivyonunua Jana

Jana nilinunua vitabu vitatu katika duka la vitabu la chuoni St. Olaf. Viwili, Two Years Eight Months and Twenty-Eight Nights cha Salman Rushdie na A Strangeness in my Mind cha Orhan Pamuk, niliviona juzi. Cha tatu, Why Homer Matters, kilichotungwa na Adam Nicolson, nilikiona hiyo hiyo jana.

Nilipoingia dukani, nilikumbuka makala niliyoisoma juzi usiku, kuhusu vitabu halisi na vitabu pepe. Makala hii, sawa na nyingine nyingi, inatafakari iwapo vitabu vya jadi vitasalimika katika himaya hii ya vitabu pepe. Lakini inahitimisha kuwa hakuna ushahidi kuwa vitabu vya jadi vitapoteza mvuto au kufifia.

Mimi ni mmoja wa wale ambao hatujabadilika. Bado tumezoea vitabu halisi, yaani vitabu vya jadi, na ndio maana sisiti kuvinunua, wala sisiti kuelezea tabia yangu hiyo. Hapa nitaelezea kifupi kwa nini nimenunua vitabu hivi vitatu.

Kitabu cha Salman Rushdie kilinivutia kwa sababu ya umaarufu wa mwandishi huyu. Bila shaka wengi watakumbuka kitabu chake, Satanic Verses, ambacho kilipigwa marufuku katika nchi nyingi kwa madai kuwa kinaukashifu u-Islam. Ayatollah Khomeini wa Iran alitangaza fatwa kuwa Salman Rushdie anapaswa kuuawa.

Duniani kote, na hata miongoni mwa wa-Islam wenyewe hukumu hii ilizua mjadala. Baadhi walisema kuwa fatwa haikupaswa kutolewa kabla ya Salman Rushdie kupewa fursa ya kujieleza na kukiri kosa lake. Watu wengine walisema kuwa zogo hili lilimpa Salman Rushdie umaarufu ambao hakustahili kwa kigezo cha ubora wa uandishi wake.

Ninavyo baadhi vitabu vya Salman Rushdie, kikiwemo hiki cha Satanic Verses. Nimemewahi kufundisha riwaya yake maarufu, Midnight's Children. Ninavutiwa na ubunifu wake katika kuelezea mambo, na uhodari wake wa kutumia lugha. Uandishi wake unasisimua na kufikirisha.

Orhan Pamuk ni mwandishi ambaye nimewahi kumtaja katika blogu hii. Nina vitabu vyake kadhaa, na nimekuwa na hamu ya kuvisoma, ila bado sijapata wasaa. Huyu amenivutia si tu kwa kuwa alipata tuzo ya Nobel, bali pia kwa sababu ninafahamu kiasi fulani kuhusu fasihi simulizi ya Uturuki, kama vile hadithi za Nasreddin Hodja na Dede Korkut.

Why Homer Matters nimekipenda kwa kuwa taaluma ya tendi nimeipenda na kuishughulikia kwa miaka mingi. Homer, ingawa taarifa zake hazijulikani vizuri, ndiye anayehusishwa na tendi maarufu za u-Griki ya kale, The Iliad na The Odyssey. Kwa kuangalia juu juu, niliona kuwa mwandishi wa Why Homer Matters ana uwezo mkubwa wa kuelezea masuala ya Homer na hizi tendi.

Sunday, September 7, 2014

Ninasoma "Shalimar the Clown," Riwaya ya Salman Rushdie.

Salman Rushdie ni mmoja wa waandishi maarufu kabisa wanaoandika katika ki-Ingereza. Kwa uandishi wake, amepata tuzo zinazoheshimika sana, kama vile "Booker Prize."

Mimi ni mwalimu wa fasihi ya ki-Ingereza. Mara moja moja ninafundisha kozi ya "South Asian Literature," yaani fasihi ya Asia ya Kusini. Katika kozi hii, ninafundisha maandishi ya watu kama Rabindranath Tagore, R. K. Narayan, Raja Rao, Mulk Raj Anand, Anita Desai, Michael Ondaatje, na Salman Rushdie.

Haiwezekani kusoma au kufundisha maandishi yote. Vile vile, kazi mpya za fasihi zinaendelea kuchapishwa. Kwa hivi, kila ninapofundisha kozi ya namna hii, najua kuwa katika orodha yangu kuna waandishi ambao hawamo. Kuna kazi muhimu za fasihi ambazo hazimo. Huu ndio ukweli, ingawa haupendezi.

Uchaguzi wowote wa waandishi au maandishi ambao ninafanya kwa kufundishia katika muhula fulani wa masomo una utata na unazua masuali. Nilipofundisha kozi ya "South Asian Literature" kwa mara ya kwanza, Salman Rushdie hakuwemo. Nilijiuliza kama hii ni sahihi.

Hatimaye, nilianza kutumia maandishi ya Rushdie. Nilianzia na riwaya yake maarufu ya Midnight's Children. Hii sio riwaya rahisi kuisoma, lakini wanafunzi wangu nami tulifanya bidii tukaimaliza. Salman Rushdie anaandika ki-Ingereza ambacho kina mvuto wa pekee, ingawa sio rahisi, kwa mbinu za kila aina. Anadhihirisha ufahamu mkubwa wa ki-Ingereza, falsafa, fasihi, dini, siasa, na tamaduni mbali mbali. Msomaji unajikuta katika kazi kubwa ya kufikiri na kukabiliana na chemsha bongo mbali mbali.

Midnight's Children ilinipa hamasa ya kutumia maandishi ya Rushdie. Muhula huu wa masomo ambao ulianza wiki iliyopita, nitatumia riwaya yake ya Shalimar The Clown. Sikuwa nimeisoma riwaya hii, bali nimeanza, katika kujiandaa kuifundisha. Panapo majaliwa, hapo tutakapokuwa tumemaliza kuisoma na kuijadili, nitaandika habari zake katika blogu hii. Ila napenda kutoa tahadhari kuwa dhana ya kumaliza kusoma kazi yoyote ya fasihi sio dhana yenye ukweli. Ingawa tunaitumia dhana hii, tunajidanganya.


Monday, June 3, 2013

Tunaanza Kusoma "Midnight's Children, Kitabu cha Salman Rushdie

Wiki kadhaa zilizopita, niliezea katika blogu hii azma yangu ya kufundisha kitabu cha Salman Rushdie kiitwacho Midnight's Children.

Sasa wakati wa kufanya hivyo umefika. Leo ni siku ya kwanza ya muhula wa kipindi cha joto. Ni siku ya kwanza ya somo langu la Post-colonial Literature. Leo nimejitambulisha kwa wanafunzi na kuitambulisha kozi.

Nimeongelea maana ya Post-olonial literature na utata uliopo katika dhana hiyo, malumbano yanayoligubika dhana hiyo.

Nimetoa utangulizi kuhusu India, historia ya utamaduni wake na fasihi yake, nikianzia na tungo za kale za Mahabharata na Ramayana, nikalipitisha darasa hadi kwenye uandishi wa watu kama Kalidasa, Tagore, Raja Rao, Mulk Raj Anand, na R.K. Narayan. Niliwaelezea jinsi, kwenye miaka ya sitini hadi leo, wanawake wamejitokeza katika uandishi wa India na wanatoa mchango mkubwa.

Hayo yote yalikuwa ni sehemu ya  matayarisho ya kusoma na kujadili Midnight's Children. Nimewaelezea kiasi habari za mwandishi Salman Rushdie, maandishi yake, na zogo lililozuka duniani baada ya yeye kuchapisha kitabu cha Satanic Verses.

Hayo niliyowaeleza leo yatakuwa yanajitokeza tena na tena wakati wa kujadili kazi za fasihi. Nimefurahi kuwajulisha wanafunzi majina ya waandishi mbali mbali. Tutakaphotimisha majadiliano kuhusu Midnight's Children, tutasoma The Guide, riwaya ya R. K. Narayan, ambaye nimemtaja leo.

Baada ya hizo kazi za fasihi ya India, tutasoma kazi kadhaa za fasihi ya Afrika, ambazo ni Half of a Yellow Sun kilichoandikwa na Chimamanda Ngozi Adichie wa Nigeria na Unconfessed kilichoandikwa na Yvette Christianse wa Afrika Kusini.

Nimewaambia wanafunzi kuwa ni kawaida yangu kuweka katika kozi yangu baadhi ya vitabu ambavyo sijawahi kuvisoma. Ninapenda changamoto ya kuvisoma sambamba na wanafunzi.

Wednesday, April 3, 2013

Nitafundisha "Midnight's Children," Kitabu cha Salman Rushdie

Nimefundisha fasihi ya India mara nyingi sana, hapa Chuoni St. Olaf, kuanzia mwaka 1991. Nimefundisha maandishi ya watu kama Rabindranath Tagore, Mulk Raj Anand, Raja Rao, R.K. Narayan, Ruth Prawer Jhabvala, Nayantara Sahgal, Anita Desai, na Kamala Markandaya.

Sijawahi kufundisha maandishi ya Salman Rushdie, ambaye ni mwandishi maarufu sana, sambamba na hao niliowataja. Suali moja ambalo nimejiuliza miaka ya karibuni ni je, utafundishaje fasihi ya India bila kumjumlisha Salman Rushdie? Utaachaje kufundisha kitabu cha Rushdie kiitwacho Midnight's Children, ambacho kilipata tuzo maarufu ya Booker?

Mwezi Juni hadi Julai nitafundisha kozi ya wiki sita, katika somo liitwalo "Post-colonial Literature." Nimeamua kufundisha kitabu hiki cha Rushdie. Ni kitabu muhimu kwa namna nyingi, sio tu kwa upande wa sanaa, bali pia kwa jinsi kinavyojumlisha masuala na dhamira mbali mbali ambazo ni muhimu katika fasihi ya India. Ni kitabu chenye upekee kihistoria na kisiasa kwa jinsi kilivyofungamana na tukio moja muhimu sana katika karne ya ishirini, yaani kupatikana kwa uhuru kwa nchi iitwayo India.

Tukio hili la uhuru wa India lilitokea mwaka 1947. Ila kwa bahati mbaya sana, ni tukio lililoandamana na mgawanyiko uliosababisha kuwepo kwa nchi mbili, yaani India na Pakistan. Ni tukio lililoandamana na uhasama, mauaji na ukimbizi wa idadi kubwa sana ya watu, mtafaruku ambao ulikuwa baina ya wa-Hindu na wa-Islam. Tukio hili linakumbukwa kwa majonzi, na limeelezwa sana na waandishi kutoka India na Pakistan.

Kwa vile kitabu cha Midnight's Children kina kurasa nyingi sana, nimeona kuwa nisiweke vitabu vingi katika kozi hii ya wiki sita.  Nawazia kutumia vitabu vingine viwili au vitatu, ambavyo navyo vina kurasa nyingi. Nimeamua tu kutumia haya mavitabu makubwa nione itakuwaje. Kimoja ninachowazia sana ni Half of a Yellow Sun, cha Chimamanda Ngozi Adichie, wa Nigeria. Kingine ni Abyssinian Chronicles cha Moses Isegawa wa Uganda. Bado nina muda wa kufikia uamuzi wa mwisho. Huenda nikatumia The Famished Road, cha Ben Okri, au Wizard of the  Crow, cha Ngugi wa Thiong'o. Uamuzi kamili nitafikia katika siku kadhaa zijazo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...