Showing posts with label Wamarekani. Show all posts
Showing posts with label Wamarekani. Show all posts

Saturday, May 8, 2010

Tamaduni Zinapogongana

Yeyote anayefuatilia blogu zangu na maandishi mengine ataona kuwa ninashughulika sana na masuala ya tofauti za tamaduni hapa duniani. Ninatoa ushauri kwa taasisi, vyuo, makampuni, na watu binafsi kuhusu masuala hayo. Ninaendesha warsha hapa Marekani na Tanzania, na ninapangia kufanya hivyo katika nchi zingine za Afrika na duniani kwa ujumla.

Haya ninayoongelea si mambo ya kinadharia tu wala ya kuyafanyia mchezo. Yasipoeleweka na kushughulikiwa ipasavyo, yanaweza kuwa na athari kubwa katika jamii na katika dunia yetu. Mifano ni mingi, nami naitaja katika warsha zangu.

Napenda kuongelea kisa kimoja kilichosababisha niitwe kwenye mji wa Faribault, Minnesota, katikati ya mwezi Aprili mwaka huu, kutatua mgogoro uliokuwa unafukuta baina ya wa-Marekani ambao ni wafanyabiashara katika mji ule na wa-Somali ambao wamehamia katika mji ule, wengi wao wakiwa ni wakimbizi.

Kwa muda mrefu kumekuwa na mgogoro kati ya jamii hizi mbili. Wa-Somali, kama ilivyo kwetu Afrika wana jadi ya kuwa wanapokutana na wenzao njiani, mitaani, au popote pale wanasimama na kuongea, aghalabu kwa muda mrefu, hata kama ni kwenye sehemu wanayopita watu. Vikundi hivi vya wa-Somali vimesababisha wafanyabiashara kupata hasara, kwani wateja wao wanaogopa. Hii ni hali halisi ya Marekani, kufuatana na historia ya mahusiano baina ya Wamarekani wazungu na Wamarekani weusi, pia taratibu zao za kutoziba njia.

Wasomali wa Faribault hawakuwa na fununu kuwa mila na desturi zao haziendani na mila na desturi za hapa Marekani. Kuziba njia, kama tunavyofanya Afrika wakati tunapokutana na kuongea na wenzetu, hairuhusiwi hapa Marekani.

Kutokana na hali hiyo, rais wa wafanyabiashara wa Faribault, Mama Kymn Anderson, akishirikiana na taasisi ya Welcome Center, walifanya mpango wa kunialika nikaongee na hao wa-Marekani na wa-Somali, tarehe 15 Aprili. Kwa wiki kadhaa waandaaji walinipa fununu kuhusu suala lililokuwa linaukabili mji wao nami nilijiwa na mawazo mengi, kwani halikuwa suala rahisi. Katika kulitafakari na kujiandaa nilipatwa na mawazo mengi, na hata niliandika ujumbe kwenye blogu yangu ya ki-Ingereza. Bofya hapa.

Siku iliwadia, nami nilienda Faribault. Tulikutana katika ukumbi wa maktaba ya Faribault. Walikuwepo watu zaidi ya ishirini, wawakilishi wa pande zote mbili. Sikuona nyuso za furaha, kutokana na hali ya mgogoro. Niliona niko katika mtihani. Nilijitahidi nilivyoweza katika hotuba yangu, na mambo yalienda vizuri. Bofya hapa.

Kwa kutambua kuwa hili lilikuwa suala linalohusu wa-Marekani na wa-Afrika, Mama Anderson alikuwa ameniagiza nichukue nakala za kitabu changu cha Africans and Americans, ambacho alishakisoma. Nilichukua nakala kadhaa ambazo, baada ya mazungumzo yangu, zilinunuliwa upesi na wengine wakakosa. Uamuzi uliofikiwa ni kuwa tutaendeleza utaratibu huu wa mazungumzo siku za usoni.

Kwa wale walioko Tanzania, nitaendesha tena warsha kadhaa mwaka huu, kuhusu utamaduni na utandawazi. Warsha ya kwanza itafanyika Tanga, tarehe 12 Juni. Kwa taarifa zaidi, bofya hapa.

Saturday, February 6, 2010

Wamarekani Safarini Malawi

Leo nilikwenda mjini Chippewa Falls, katika jimbo la Wisconsin, umbali wa maili 123 kutoka Northfield, ambapo naishi. Nilienda kuongea na kikundi cha wa-Marekani wanaojiandaa kwenda Malawi kwa shughuli za kujitolea. Nilialikwa na Mama Diane Kaufmann, ambaye anaonekana kushoto kwangu, katika picha hapa juu. Yeye ameenda Malawi mara kadhaa, katika wadhifa wake kama mratibu wa mpango wa ushirikiano baina ya dayosisi ya Kanisa la kiLuteri Kaskazini Magharibi ya Wisconsin na Malawi. Ana uzoefu wa kupeleka vikundi vya wanadayosisi Malawi katika mpango huo. Vile vile tumeshirikiana kwa miaka kadhaa katika kuendesha mafunzo kwenye kituo cha Luther Point.
Kikundi nilichoenda kukutana nacho leo kinaenda Malawi kuwashughulikia watu wenye matatizo ya macho, na kuwagawia miwani. Wanatarajia kufanya shughuli hizo Karonga na Chitipa.
Baadhi yao wameshaenda Malawi, na kwa wengine hii itakuwa ni mara yao ya kwanza. Mama Kaufmann aliniita niongee nao kuhusu masuala ninayoongelea katika kitabu changu cha Africans and Americans. Alinieleza kabla kuwa washiriki wote watakuwa wamekisoma kitabu hiki kabla ya ujio wangu. Kama kawaida, mazungumzo na watu waliojiandaa namna hii yanakuwa ya kina, kwani yanalenga katika kufuatilia yale ambayo wamesoma.
Walifurahi kuwa nami, kwani walijisikia kama vile wameshanifahamu, kutokana na ninavyojieleza kitabuni. Nami nilifurahi kuwa nao na kuwasisitizia mambo ya msingi kuhusu kuishi au kushughulika na watu wa utamaduni tofauti na wetu. Kwa vile hao wanaenda kwa shughuli za matibabu, mazungumzo yetu yalilenga zaidi kwenye hali halisi ya kushughulika na watu katika hospitali. Tofauti za tamaduni zinajitokezaje katika mazingira ya hospitali.
Kwa bahati nzuri haya ni mambo ambayo nimeyawazia kwa muda mrefu, na katika kitabu changu nimeyagusia. Vile vile, nimekuwa nikijipatia uzoefu katika mazungumzo na wanafunzi wa masomo ya uuguzi wanapojiandaa kwenda Tanzania kimasomo.

Baadhi ya wasafiri hao walisoma katika chuo cha St. Olaf, na tulipata fursa ya kuongelea na kupiga soga kuhusu maisha chuoni hapa. Baadhi wamesoma maandishi yangu mengine, kama vile Matengo Folktales na Notes on Achebe's Things Apart. Niliona wazi kuwa hao ni watu makini ambao wanajishughulisha kufahamu habari za huko waendako.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...