Showing posts with label Patrick Hemingway. Show all posts
Showing posts with label Patrick Hemingway. Show all posts

Wednesday, January 11, 2017

Zawadi Kutoka Ramble Pictures Kwa Heshima Ya Hemingway

Wiki iliyopita nimepata zawadi ya picha kutoka Ramble Pictures, kampuni ya kutengeneza filamu. Kampuni hiyo ndiyo iliyotengeneza filamu ya Papa's Shadow, inayohusu maisha na safari za mwandishi maarufu Ernest Hemingway Afrika Mashariki, pamoja na maandishi yake kuhusu Afrika Mashariki. Sehemu kubwa ya filamu hiyo ni mazungumzo baina ya Mzee Patrick Hemingway na mimi, kuhusu masuala hayo.

Picha niliyopewa inaitangaza filamu ya Papa's Shadow. Inamwonesha Ernest Hemingway, Patrick Hemingway na mimi, Kuna pia Mlima Kilimanjaro na nchi tambarare chini ya mlima, na pia ndege ikiwa angani. Hiyo picha ya mlima na mazingira yake, pamoja na ndege, inakumshia hadithi maarufu ya Hemingway, "The Snows of Kilimanjaro."

Nimeguswa na picha hii. Ni heshima kubwa kuliko ninavyostahili kuwekwa sambamba na Ernest Hemingway na Patrick Hemingway. Ernest Hemingway alileta mapinduzi katika uandishi na alitunukiwa tuzo ya Nobel katika fasihi mwaka 1954. Patrick Hemingway ni mtu muhimu kwa watafiti wa Hemingway, akiwa ni mtoto pekee aliye bado hai wa Ernest Hemingway. Ametoa na anaendelea kutoa mchango mkubwa wa kuhariri maandishi ya Hemingway na kuyaandikia utangulizi.

Kwa upande mwingine ninafurahi kuoneshwa pamoja na Patrick Hemingway, ambaye ni mtu wa karibu kwangu. Ananifundisha mengi kuhusu Afrika Mashariki ya wakati alipoishi kule, kuhusu maisha na uandishi wa Hemingway, na kuhusu waandishi wengine, hasa wa wakati wa Hemingway.

Vile vile, Patrick Hemingway anakipenda sana kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Hata katika filamu ya Papa's Shadow, anakitaja, na kuna mahali anasoma kisehemu cha kitabu hiki kwa ki-Swahili na tafsiri yangu ya ki-Ingereza.

Filamu ya Papa's Shadow inaelezea upande wa Ernest Hemingway ambao haufahamiki vizuri, yaani jinsi alivyovutiwa na Afrika kwa maisha yake yote. Katika kufanya utafiti juu ya Hemingway na kusoma maandishi yake kwa miaka kadhaa, niligundua kuwa aliipenda Afrika tangu alipokuwa mtoto. Ndipo nikaamua kutunga kozi kuhusu mada hiyo.

Mwanafunzi mmoja katika kozi hiyo, Jimmy Gildea, alipata motisha ya kutengeneza filamu, na matokeo yake ni Papa's Shadow. Pamoja na kuelimisha juu ya uhusiano wa Hemingway na Afrika, filamu hii inaitangaza Tanzania. Nakala za filamu hii zinapatikana kwa kuwasiliana na Ramble Pictures kwa barua pepe: info@ramblepictures.com au kwa simu (952) 426-5809.

Sunday, May 22, 2016

Leo Nimemwandikia Mzee Patrick Hemingway

Leo nimemwandikia barua pepe Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliye hai wa mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Nilipiga naye picha inayoonekana hapa kushoto tarehe 27 Aprili, 2013, nyumbani pake mjini Craig, katika jimbo la Montana.

Nilifahamu habari zake kwa miaka mingi kabla ya kufahamiana naye na halafu tukakutana. Ni mzee mwenye maongezi ya kusisimua kuhusu baba yake Ernest Hemingway na waandishi wengine wa wakati wake. Pia ana kumbukumbu nyingi za Tanganyika, na kisha Tanzania, ambako aliishi kwa miaka yapata 25 kabla ya uhuru na baada ya uhuru, akiendesha kampuni ya utalii, na hatimaye akiwa mkufunzi katika Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori cha Mwika.

Tangu tulipoanza kufahamiana, ameguswa na ari yangu ya kutafiti maandishi, falsafa, na maisha ya Ernest Hemingway, na amevutiwa na msimamo wangu kuwa Ernest Hemingway ni mwandishi aliyetuenzi sana sisi watu wa Afrika Mashariki, na tunapaswa kujielimisha kuhusu mchango wake, na kisha kuutumia katika kujitangaza kama alivyotutangaza.

Hayo yamemfanya Mzee Patrick Hemingway awe tayari kunisaidia kwa dhati katika juhudi zangu za kujielimisha na kuuelimisha ulimwengu juu ya Ernest Hemingway. Miezi kadhaa iliyopita, nilivyomweleza kuwa napangia kutembelea hifadhi ya Ernest Hemingway katika John F. Kennedy Library, aliniambia kuwa nitakapokuwa tayari nimfahamishe ili anitambulishe kwa wahusika.

Nilipoongea naye tarehe 19 mwezi huu na kumtajia tarehe nilizopangia kwenda kwa shughuli hiyo, aliniagiza nimpelekee maelezo yangu kwa barua pepe, ili aweze kuandaa utambulisho huo. Aliniambia kuwa ninakwenda wakati mzuri, kwani kuna maonesho maalum juu ya Hemingway, ambayo yameanza siku chache zilizopita na yatadumu kwa miezi kadhaa.

Basi, leo nimemwandikia. Kilichobaki sasa ni kuandaa safari, nikajionee hiyo hifadhi kubwa kuliko zote duniani juu ya Ernest Hemingway. Hii itakuwa ni mara yangu ya kwanza kuitembelea hifadhi hiyo, lakini sitegemei kuwa itakuwa ni mara ya mwisho.

Wednesday, May 18, 2016

Muhula Unaisha; Umebaki Utafiti

Jana tumemaliza muhula wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Nilikuwa ninafundisha "Folklore," Muslim Women Writers, na "First Year Writing." Kwa utaratibu wa chuo hiki, masomo matatu kwa muhula ndio kiwango cha juu kabisa. Hatufundishi zaidi ya masomo matatu. Kwa hivi, nilitegemea ningekuwa nimechoka, lakini sisikii uchovu. Alhamdulillah.

Kwa wiki nzima inayokuja, tutakuwa na mitihani. Baada ya hapo tutaanza likizo ndefu ya miezi mitatu na kidogo. Inaitwa likizo, lakini maprofesa tunaona ni wakati muafaka wa kufanya shughuli za kitaaluma kama utafiti na uandishi.

Nami nimeamua kwenda Boston kwa siku chache kufanya utafiti juu ya Ernest Hemingway katika maktaba ya John F. Kennedy. Humo kuna hifadhi kubwa kuliko zote duniani ya vitabu, miswada, picha na  kumbukumbu zingine zinazomhusu Hemingway. Ingawa nimefika Boston mara kadhaa, sijawahi kwenda katika maktaba hiyo maarufu.

Nina bahati kuwa ninafahamiana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway ambaye bado yuko hai. Yeye ndiye mmiliki wa haki zote za urithi wa Hemingway. Nilipomwambia kwa mara ya kwanza kwamba napangia kwenda kufanya utafiti katika maktaba ya John F. Kennedy,  aliniambia nimfahamishe ni lini ili anitambulishe kwa wahusika. Wiki chache zilizopita, katika maongezi yetu, nilimwambia tena kuwa napangia kwenda kwenye maktaba ile, alikumbushia kuwa nimweleze ni muda upi nitakwenda ili awafahamishe.

Ninashukuru sana kwa hilo, kwani katika kusoma taarifa za maktaba ile, nimefahamu kuwa kuna masherti yanayohusu kuitumia hifadhi ya Ernest Hemingway. Mtu hukurupuki tu ukafika pale na kufanya utafiti. Kuna baadhi ya kumbukumbu ambazo zimefungiwa. Mtafiti unahitaji kibali maalum kuweza kuzifanyia utafiti. Sherti nichukue hatua hima.

Sunday, March 20, 2016

Tukio Katika Nyumba ya Hemingway, Oak Park

Tarehe 27 Februari, nilizuru nyumba alimozaliwa mwandishi Ernest Hemingway, na pia jumba la kumbukumbu ya Hemingway, kama nilivyoandika katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza. Ilikuwa ni siku ya pekee, siku ambayo ndoto yangu ya miaka ilitimia.

Kati ya watu niliokutana nao katika nyumba ya Hemingway, ambao nao walikuwa wamekuja kuitembelea, ni binti aliyejitambulisha kuwa ni wa ukoo wa Hemingway. Alinipa kadi yake, iliyoonyesha kuwa jina lake ni Laura Hemingway.

Nilishangaa na kufurahi, nikaanza kuongelea namna ninavyomwenzi Hemingway. Niliongelea kozi yangu ya Hemingway, na jinsi ninavyowasiliana na mzee Patrick Hemingway. Binti huyu na wengine tuliokuwa tunasubiri kuanza ziara walivutiwa na taarifa hizo. Ninajitambua kuwa siwezi kuiachia fursa yoyote ya kuongelea habari za Hemingway.

Kwa bahati mbaya, niliporejea kutoka Chicago, niligundua kuwa nilikuwa nimepoteza anwani ya binti huyu. Leo amejitokeza katika facebook kuanzisha mawasiliano nami. Baada ya kuweka uhusiano huo, nimeweza kuipata picha tuliyopiga siku tulipokutana, ambayo inaonekana hapa juu.

Monday, December 7, 2015

Nimesaini Vitabu Kwa Ajili ya Filamu ya "Papa's Shadow"

Wakati wa kampeni ya Ramble Pictures ya kuchangisha fedha kulipia gharama za filamu ya Papa's Shadow, nilichangia fedha kiasi na pia nakala za kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Walikuwa wameweka viwango mbali mbali vya michango ambavyo viliendana na vizawadi na vivutio kwa wachangiaji. Waliochangia dola 200 au zaidi waliahidiwa nakala ya kitabu changu kama zawadi.

Leo, Jimmy Gildea, mwanzilishi wa Ramble Pictures na mtengenezaji wa Papa's Shadow, ambaye alikuwa mwanafunzi katika kozi yangu ya Hemingway, alinifuata hapa chuoni St. Olaf, nikasaini nakala tano za kitabu changu, na kumkabidhi.

Tulipata fursa ya kuongelea habari za Ernest Hemingway, ziara yetu ya Montana, msisimko na mafanikio ya kampeni ya kuchangisha fedha, na kadhalika. Vile vile, Jimmy alinirekodi nikiwa nasoma kitabu cha Green Hills of Africa na pia nikiwa natembea katika sehemu iliyoonyesha vizuri mandhari ya chuo. Jimmy aliniuliza iwapo nina picha za ujana na utoto wangu. Anakusanya hayo ili kuyatafutia nafasi katika filamu ya Papa's Shadow, ingawa tayari ni nzuri sana, kwa jinsi nilivyoiona.

Papa's Shadow inategemewa kupatikana wiki chache kuanzia sasa, labda mwezi Februari. Si filamu ya kuigiza bali ni mazungumzo juu ya maisha, uandishi, na falsafa, ya Ernest Hemingway, hasa inavyohusiana na safari zake Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54. Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye bado hai. Ni filamu inayoelimisha, si burudani.

Tuesday, October 13, 2015

Michango ya Papa's Shadow Imekamilika

Kwa mwezi mzima kumekuwa na kampeni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya filamu ya Papa's Shadow, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Leo, shughuli imekamilika, masaa sita kabla ya kipindi cha michango kwisha.

Mafanikio haya yamefungua njia kwa mambo makubwa siku zijazo. Papa's Shadow sasa itapatikana kwa wadau, pindi taratibu za malipo zitakapokamilika. Kwangu ni furaha kubwa, kama mchangiaji mkuu wa filamu hiyo, sambamba na Mzee Patrick Hemingway, wa maelezo na uchambuzi juu ya mwandishi Ernest Hemingway. Ninafurahi pia kwamba filamu hii itaitangaza Tanzania kwa namna ya pekee, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Umaarufu wa Ernest Hemingway ulimwenguni ni wa pekee. Pamoja na kuelezea uhalisi wa maisha ya binadamu, kama walivyofanya waandishi wengine maarufu, pamoja na kuzipa umaarufu kwa maandishi yake sehemu alizotembelea hapa duniani, Hemingway alianzisha jadi mpya kimtindo katika uandishi wa ki-Ingereza. Hilo limesemwa tena na tena na wataalam wa fasihi. Ninaamini kuwa Papa's Shadow itahamasisha ari mpya ya kusoma maandishi ya Hemingway.

Ninafurahi kuwa, katika Papa's Shadow, nimechangia kuleta mtazamo mpya juu ya Hemingway, na kuelekeza mawazo ya wasomaji na wapenzi wa Hemingway upande wa Afrika Mashariki, na hasa Tanzania. Wote waliochangia mradi huu kwa namna moja au nyingine, kwa hali na mali, wana sababu na haki ya kujipongeza.

Friday, October 9, 2015

Nimepata Toleo Jipya la "Green Hills of Africa"

Leo ni siku ya furaha kwangu. Nimepata nakala ya toleo jipya la Green Hills of Africa, kitabu cha Ernest Hemingway, kilichochapishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1935. Taarifa kwamba toleo hili lilikuwa linaandaliwa nilielezwa na Mzee Patrick Hemingway, kama nilivyoandika katika blogu hii. Kwa hivi, nilipogundua kwamba limechapishwa, niliagiza nakala hima.

Katika Green Hills of Africa, Hemingway anaelezea mizunguko yake katika nchi ya Tanganyika, mwaka 1933-34, akiwa na mke wake wa pili Pauline Pfeiffer. Anaelezea uzuri wa nchi, watu wa makabila, tamaduni, na dini mbali mbali, na wanyama katika mbuga alimowinda, kama vile Serengeti na eneo la Ziwa Manyara. Anaelezea miji alimopita, kama vile Mto wa Mbu, Babati, Kondoa, Handeni, na Tanga.

Toleo hili la Green Hills of Africa lina mambo ambayo hayakuwemo katika toleo la mwanzo, kama vile maandishi ya awali ambayo hayakutokea kitabuni, picha, na hata "diary" aliyoandika Pauline alipokuwa safarini na mumewe. Nilijua kuwa "diary" hii imehifadhiwa katika maktaba ya Chuo Kikuu cha Stanford, na nilikuwa nawazia kwenda kuisoma. Kuchapishwa kwake katika toleo hili ni jambo la kufurahisha sana.

Kutokana na jinsi Hemingway alivyoielezea nchi yetu, tukio la kuchapishwa kwa toleo hili la Green Hills of Africa mwaka huu ilipaswa tulipokee kwa shamra shamra. Pangekuwa na shughuli za uzinduzi wa toleo hili, makongamano, na tahakiki magazetini. Nakala zingejaa katika maduka ya vitabu, na wateja wangekuwa wanapigana vikumbo kuzinunua.

Sehemu zingine duniani wanatumia vilivyo bahati ya kutembelewa na Hemingway na kuandikwa katika maandishi yake. Ni kivutio kikubwa kwa watalii, kama ninavyosema katika blogu hii. Sisi tumeifanya nchi yetu kuwa kwenye miti ambako hakuna wajenzi.

Saturday, September 26, 2015

Nimehojiwa Kuhusu Hemingway na "Papa's Shadow"

Leo nimekuwa na mahojiano na mwandishi wa gazeti la Manitou Messenger linalochapishwa hapa chuoni St. Olaf. Ni gazeti la wanafunzi, ambalo limekuwa likichapishwa kila wiki kwa miaka 125. Mahojiano yetu yalikuwa juu ya filamu ya Papa's Shadow. Katika ujumbe wa kuomba mahojiano, mwandishi aliandika:

...we are doing a feature article this week on the documentary, Papa's Shadow and Ramble Pictures. We learned that you were instrumental in the inspiration for and production of this film, and we were hoping you could answer a few quick questions.

Katika mahojiano, tumeongelea nilivyoanza kuvutiwa sana na mwandishi Ernest Hemingway, nilipoombwa na Thomson Safaris kuongoza msafara mkubwa wa wanafunzi, wazazi na walimu, katika safari ya Tanzania mwaka 2002. Hatimaye, baada ya miaka mitano ya kusoma maandishi na habari za Hemingway, nilitunga kozi Hemingway in East Africa, kwa ajili ya Chuo cha Colorado.

Baadaye, niliona niunde kozi hiyo kwa ajili ya wanafunzi wa Chuo cha St. Olaf. Nilifanya hivyo mwaka 2012. Wakati wa kuandikisha wanafunzi, alinifuata kijana aitwaye Jimmy Gildea, akaniomba nimruhusu kujiunga na kozi, kwa kuwa alimpenda Hemingway na alitaka kurekodi filamu ya kozi. Nilimsajili katika darasa.

Kozi ilikwenda vizuri, kama nilivyoandika hapa. Baada ya kurejea tena Marekani, baadhi yetu tulifunga safari ya jimbo la Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Tuliongea naye sana.

Jimmy alikuwa amenirekodi ofisini mwangu nikizungumza juu ya Hemingway, akachanganya mazungumzo haya na yale tuliyofanya na Mzee Patrick Hemingway,na akaongezea mambo mengine aliyorekodi Tanzania. Kwa bahati nzuri, tulipomaliza kozi, familia ya Jimmy walikuja kumchukua wakaenda kupanda Mlima Kilimanjao. Papa's Shadow inaonyesha safari yao ya kupanda mlima. Ni rekodi nzuri sana. Ninaamini itawavutia watalii.

Kuna mambo mengine niliyomwambia huyu mwandishi wa Manitou Messenger. Hasa, nilisisitiza azma yangu ya kuendelea kufanya kila juhudi kuuelimisha ulimwengu juu ya namna Hemingway alivyoipenda Afrika na namna maisha yake na fikra zake zlivyofungamana na Afrika. Nilimwambia pia kuwa Jimmy ni mfano murua wa kuigwa na wahitimu wengine wa vyuo. Alifuata na anaendelea kufuata anachokipenda moyoni mwake, yaani kutengeneza filamu za kuelimisha. Yeye na vijana wenzake katika Ramble Pictures wanajituma kwa roho moja katika shughuli zao na hawatetereshwi na magumu au vipingamizi vyovyote.

Thursday, September 24, 2015

"Papa's Shadow" Yapongezwa na Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa

Tarehe 20 mwezi huu nilipeleka ujumbe Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa kuhusu filamu ya Papa's Shadow. Sikuandika ujumbe mrefu, bali niliwatumia kiunganishi hiki.

Bila kuchelewa, tarehe 22 nilipata ujumbe kutoka kwao, ukiwa umeandikwa na Ndugu Noel Kabanda. Uwakilishi unaafiki kuwa Papa's Shadow ni "fursa maridhawa ya kuitangaza Tanzania ulimwenguni" na unasisitiza kuwa "Serikali inatambua mchango wa sanaa katika kuitangaza Tanzania katika sekta mbali mbali ikiwemo utalii na utamaduni."

Kwanza, kwa kuzingatia uwingi wa majukumu yanayowakabili wawakilishi wetu katika balozi zetu, nimeona ni muhimu kusema nilivyoguswa na jinsi Uwakilishi ulivyoushughulikia ujumbe wangu.

Pili, ujumbe wa Uwakilishi unawatia moyo wahusika wa Ramble Pictures, ambao ndio watengeneaji wa Papa's Shadow. Timu nzima ya Ramble Pictures ni vijana wa ki-Marekani, na baadhi yao walikuja Tanzania mwaka 2013 kwenye kozi yangu ya Hemingway Katika Afrika Mashariki. Ni furaha kwangu, na jambo la kujivunia, kuwaeleza vijana hao kuwa Uwakilishi wa Kudumu waTanzania Umoja wa Mataifa umeipokea Papa's Shadow kwa namna hii.

Papa's Shadow si filamu ya maigizo. Ni filamu ya kuelimisha kuhusu mwandishi Ernest Hemingway. Sehemu kubwa ya filamu hiyo ni maongezi baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa mwandishi Hemingway. Tunaongelea maisha ya Hemingway, safari zake, uandishi wake, na fikra zake kuhusu masuala mbali mbali. Tunawafungua macho walimwengu kuhusu namna Hemingway alivyoipenda Afrika na alivyokuwa mtetezi wa Afrika.

Hemingway alisafiri na kuishi Afrika Mashariki mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54. Aliandika hadithi, insha, barua na maandishi mengine ambayo ni hazina kubwa. Wenzetu katika nchi zingine ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari za huko, wametumia fursa hiyo kujitangaza, na wanawavutia watalii wengi sana. Mifano ni miji kama Paris (Ufaransa), Havana (Cuba), Oak Park (Illinois, Marekani), Key West (Florida, Marekani), na Pamplona (Hispania). Hemingway anapendwa ulimwenguni kote ambako watu wana utamaduni wa kusoma vitabu. Sina shaka kuwa Papa's Shadow italeta msisimko wa aina hiyo kwa kuwaelekeza mashabiki wa Hemingway nchini kwetu.

Hamu ya kuona Tanzania inafunguka macho kuhusu fursa hii ilinihamasisha kufanya utafiti juu ya safari za Hemingway katika nchi yetu na maandishi aliyoandika. Kozi niliyotunga ilikuwa na lengo hili. Nilitaka pia kuwasaidia walimwengu kuelewa umuhimu wa Afrika katika maisha na uandishi wa Hemingway. Kwa msingi huo huo, nilishiriki kikamilifu katika kufanikisha filamu ya Papa's Shadow.

Nimeeleza hayo yote ili kuweka wazi umuhimu wa ujumbe wa Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa. Ni mfano wa mshikamano unaotakiwa baina yetu wanadiaspora, serikali, na wananchi wenzetu.

Wednesday, September 16, 2015

Filamu ya "Papa's Shadow:" Fursa ya Kuitangaza Tanzania

Nina furaha kuandika kuhusu filamu ambayo imeandaliwa iitwayo "Papa's Shadow," inayomhusu mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Katika filamu hiyo, ninaonekana nikiongea na Mzee Patrick Hemingway, ambaye ni mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye hai. Ana umri wa miaka 87. Tunaongelea maisha, safari, maandishi na fikra za Hemingway, hasa kuhusu Afrika.

Sehemu nyingi hapa duniani ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari zake, zimejipatia umaarufu. na zinafaidika hasa katika utalii. Mifano ni Cuba na mji wa Pamplona nchini Hispania. Watu wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla tuna bahati hiyo, kwani Hemingway alikuja na kuishi kwetu mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54, akaandika vitabu, hadithi, insha na barua kuhusu aliyoyaona.

Filamu ya "Papa's Shadow" ilitokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013 juu ya Hemingway. Kozi ile ilimhamasisha Jimmy Gildea, mmoja wa wanafunzi wangu, kutengeneza filamu hiyo. Alianzisha kampuni, Ramble Pictures, akaanza kutegeneza hiyo filamu ya kuelimisha. Anaendelea kutengeneza filamu zingine zenye kuelimisha.

"Papa's Shadow" inaitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Kuna kampeni ya kuchangisha fedha za kumalizia malipo ya usajili na taratibu zingine kabla ya filamu kuonyeshwa na kusambazwa. Naleta hapa ujumbe ambao umeandikwa na binti yangu Zawadi, mmoja wa watu wanaojitolea katika Ramble Pictures, unaoelezea kampeni hiyo.

Nitapenda ujumbe huu uwafikie wa-Tanzania popote duniani, hasa wanadiaspora, ofisi za ubalozi, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, na wadau wengine wote. Nilitumia miaka kadhaa kusoma maandishi ya Hemingway na kuandaa kozi ambayo ni chimbuko la filamu hii. Ninapangia kuendelea kufundisha kozi hiyo. Nawe m-Tanzania mwenzangu una fursa ya kutoa mchango wako. Tushirikiane. Tutafanikiwa. Sisi tuliokuwepo wakati Tanganyika ilipopata Uhuru tunakumbuka kauli mbiu ya Mwalimu Nyerere ya kuhimiza maendeleo ya Taifa jipya: "It can be done; play your part."

=====================================================

Hello!

My name is Zawadi Mbele, and I am contacting you today to let you know about an amazing project. Ramble Pictures, a Minneapolis-based, independent film company, recently launched a 30-day "Kickstarter" campaign in order to raise funds for the distribution of our completed documentary, Papa's Shadow.

Papa's Shadow is a personal film about Ernest Hemingway in East Africa. It explores his hunting expeditions and holds key dialogues on subjects such as race, language, and the cultures that distinguish us as citizens of the world. Featuring exclusive testimony by Ernest's only living son, Patrick Hemingway, as well as Tanzanian author and Hemingway scholar, Dr. Joseph Mbele, this documentary explores the integral role of two safaris in their shaping of an author and demise of a legend. 

Over the past four years, hard work and creative energy has been poured into making this feature-length documentary. The film has already been completed, however, we cannot show or distribute the film until we finish paying for copyright licensing. Again, please visit our Kickstarter webpage to learn more about how you can play an important role in bringing this documentary to distribution. Also, with Kickstarter, we are offering exclusive rewards with every donation, such as the new Hemingway Library Edition of "Greens Hills of Africa," signed by Patrick Hemingway. 

If there is someone else from your organization you would recommend contacting, we would be grateful to have our information passed along. If you can, please take the time to explore our webpage and let me know if you have any questions at all. You can email me directly or email Elizabeth Turner at elizabeth@ramblepictures.com.

Thank you for your time, and we look forward to hearing back from you!

Sincerely,

Zawadi Mbele
email: zawadi.mbele@gmail.com

Wednesday, September 9, 2015

Vijana Wameonana Na Mzee Patrick Hemingway

Leo nimepata ujumbe na picha kutoka kwa Jimmy Gildea, anayeonekana kushoto kabisa pichani hapa kushoto, kwamba walikuwa mjini Bozeman, Montana, wakingojea kuonana na Mzee Patrick Hemingway na mkewe Mama Carol.

Jimmy alikuwa ni mmoja wa wanafunzi wangu katika kozi ya Hemingway in East Africaambayo nilifundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013. Kutokana na kozi ile, na pia safari tuliyofunga kwenda Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, Jimmy ametengeneza filamu iitwayo Papa's Shadow, ambayo kwa kiasi kikubwa inatokana na kozi ile.

Katika filamu hii, ambayo si ya maigizo, Mzee Patrick Hemingway na mimi tunaongelea maisha na maandishi ya baba yake, Ernest Hemingway, na tunaongelea kwa undani zaidi maisha na mizunguko yake Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54, na pia falsafa yake kuhusu masuala ya maisha na uandishi. Katika kutengeneza filamu hiyo, Jimmy ameshirikiana na hao vijana wanaoonekana pichani, na wengine ambao hawamo pichani.

Nimetamani sana kama nami ningekuwa Bozeman leo kuonana na Mzee Patrick Hemingway na Mama Carol. Hata hivi, nafarijika kwamba ninampigia simu wakati wowote nikipenda. Kwa kuwa aliishi miaka yapata 25 Tanganyika (na hatimaye Tanzania), ameniambia kuwa anafurahi kuongea na mimi, kwa kuwa hana watu wa kuongea nao kuhusu Tanzania na Afrika.

Kwa upande wangu, najifunza mengi kutoka kwa Mzee Patrick Hemingway, juu ya Ernest Hemingway, waandishi wengine, historia ya Tanganyika, na mambo mengine mengine. Pia ninaguswa kwa jinsi anavyokipenda kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Hata katika filamu ya Papa's Shadow anakitaja na kukinukuu. Katika hiyo picha ya pili, tuliyopiga nyumbani mwake mjini Craig, Montana, anaonekana Mzee na Mama Carol Hemingway, na kitabu kiko mezani hapo mbele yake.

Monday, August 10, 2015

Bendera ya Tanzania Itapepea Faribault, Minnesota, 22 Agosti

Tarehe 22 Agosti, nitashiriki tamasha la kimataifa mjini Faribault, Minnesota. Nimeshalipia gharama. Nitakuwa na meza ambapo nitaweka vitabu vyangu na machapisho mengine.

Hapo nitaongea na watu siku nzima kuhusu shughuli zangu za ufundishaji, utafiti, uandishi, na utoaji ushauri kuhusu athari za tofauti za tamadauni, ushauri ambao ninautoa kwa wanafunzi na waalimu wa vyuo vya Marekani na watu wengine waendao Afrika, taasisi na jumuia zenye mahusiano na wa-Afrika, na kadhalika.

Nitaweka pia mabango ya filamu ya "Papa's Shadow." Filamu hiyo, ambayo ni ya maelezo ("documentary"), kwa kiasi kikubwa ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliyebaki. Tunajadili maisha na maandishi ya Ernest Hemingway, hasa yale yanayohusu Afrika. Filamu hii itaanza kuonyeshwa hivi karibuni katika majumba ya sinema na itakuwa inapatikana katika DVD na kadhalika. Kwa taarifa zaidi tembelea tovuti ya Ramble Pictures.

Jambo jingine la pekee ni kuwa, kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa tamasha la kimataifa mjini Faribault, bendera ya Tanzania itapepea, sambamba na bendera za mataifa mengine. Siku chache zilizopita, nilipeperusha bendera hii katika tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Ninapokuwa Tanzania, ninaweza kuiangalia bendera ya Tanzania nikawa ninaguswa kwa namna fulani, lakini hisia hizo huwa za pekee zaidi huku ughaibuni. Ingekuwa natoka Dar es Salaam kwenda kushiriki tamasha Mtwara, Chake Chake au Mbeya nisingeona sababu ya kubeba bendera ya Tanzania, labda kama tamasha ni la kimataifa. Na hata ningebeba, watu hawangekuwa na duku duku nayo au mshangao. Ni kitu walichozoea.

Lakini mambo ni tofauti huku ughaibuni. Sina namna ya kuelezea vizuri ninachomaanisha. Labda kwa kuwa niko mbali, nina hisia za pekee kuhusu kijiji changu cha Lituru, kata yangu ya Litembo, wilaya yangu ya Mbinga, mkoa wangu wa Ruvuma, na nchi yangu ya Tanzania.

Isipokuwa, jambo moja ni wazi, na linaelezeka: watu watakaohudhuria tamasha mjini Faribault wataiona bendera ya Tanzania. Bendera hii itatokea katika picha mbali mbali watakazopiga siku hiyo na kuzihifadhi, kuwapelekea marafiki au kuziweka mitandaoni.

Wednesday, April 22, 2015

Filamu Inayoongelea Kozi Yangu Ya Hemingway

Leo, Jimmy Gildea, mmoja wa wanafunzi waliofika Tanzania mwezi Januari 2013, kwenye kozi yangu ya Hemingway in East Africa ameniletea nakala ya awali ya Papa's Shadow, filamu ambayo ameitengeneza kutokana na kozi ile. Nimeiangalia leo hii na binti yangu Zawadi, na tumeifurahia.

Wakati nilipokuwa nawachagua wanafunzi wa kuwepo katika kozi hii, Jimmy aliomba awemo katika msafara wetu ili akarekodi kumbukumbu ("documentary"). Alikuja na vifaa vyake, akawa anarekodi matukio na sehemu mbali mbali tulizotembelea, kama vile Arusha mjini, hifadhi za Ngorongoro na Serengeti, Karatu, na Longido.

Baada ya kozi kwisha, wazazi wa Jimmy, kaka yake na dada yake walifika kumchukua Jimmy wakaenda kupanda Mlima Kilimanjaro. Filamu inaonyesha safari hiyo pia, sambamba na maneno maarufu ya Hemingway aliyoyaweka mwanzoni mwa hadithi yake maarufu, The Snows of Kilimanjaro:

Kilimanjaro is a snow-covered mountain 19,710 feet high, and is said to be the highest mountain in Africa. Its western summit is called the Masai "Ngaje Ngai," the House of God. Close to the western summit there is the dried and frozen carcass of a leopard. No one has explained what the leopard was seeking at that altitude.

Jimmy alikuwemo katika safari yangu ya Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway. mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Pichani hapo kushoto tunaonekana nyumbani kwa Mzee Hemingway katika mji wa Craig. Kuanzia kushoto ni Clay Cooper, Jimmy, Mzee Hemingway, na mimi. Clay alikuwa mmoja wa wanafunzi waliokuja kwenye kozi yangu Tanzania.

Pamoja na yote hayo, filamu inajumlisha pia sehemu alipozaliwa Ernest Hemingway, yaani Oak Park, na sehemu alipofia na kuzikwa, jimbo la Idaho. Filamu ina maelezo mengi ya Mzee Patrick Hemingway na mimi kumhusu Ernest Hemingway na maandishi na fikra zake. Jimmy aliwahi kunihoji kabla ya safari yetu ya Montana, na amejumlisha mengi niliyoyasema katika mahojiano yale.

Filamu hii ni kumbukumbu nzuri sana. Kwa namna ya pekee, inaitangaza Tanzania na Mlima Kilimanjaro, na inaitangaza kozi yangu, ambayo lengo lake lilikuwa kuuelimisha ulimwengu kuhusu jinsi Ernest Hemingway alivyoandika kwa umakini, ufahamu, na upendo mkubwa kuhusu watu wanyama, na mazingira kama alivyoshuhudia katika safari na kuishi kwake Afrika Mashariki miaka ya 1933-34 na 1953-54.

Kuna sehemu katika filamu ambapo Mzee Patrick Hemingway anakitaja kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho anakipenda, na tunamwona akisoma sehemu ya kitabu hicho, ukurasa 89, ambayo nimenukuu makala ya Ronald G. Ngala, iliyoandikwa kwa ki-Swahili. Mzee Patrick Hemingway anasoma nukuu hii pamoja na tafsiri yangu.

Ingawa tulimshuhudia Mzee Patrick Hemingway akisoma, mimi kama mwandishi wa kitabu hiki nimeguswa kuona tukio hili limo katika filamu. Baada ya kazi ngumu ya zaidi ya miaka miwili, filamu imekamilika, na inategemewa kupatikana siku za karibuni. Nitaleta taarifa.

Thursday, February 12, 2015

Kitabu Kimetimiza Miaka Kumi

Kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimetimiza miaka kumi tangu nilipokichapisha, tarehe 5 Februari, mwaka 2005. Siku hiyo niliuingiza muswada katika mtandao wa lulu nikalipia namba ya utambulisho wa kitabu, yaani ISBN. Siku hiyo hiyo niliagiza nakala ya kwanza, nikaipata baada ya wiki moja hivi. Wiki hii ni kumbukumbu ya miaka kumi ya kuwepo kwa kitabu hiki.

Mambo mengi yametokea katika miaka hii kumi kuhusiana na kitabu hiki. Nimepata fursa ya kusikia maoni ya wasomaji wengi. Baadhi wameandika maoni hayo na kuyachapisha, kama vile katika tovuti, blogu, na majarida. Wengine wameniandikia maoni yao katika barua pepe. Wengine wamenieleza maoni yao katika maongezi ya ana kwa ana.

Watu waliotoa maoni yao kuhusu kitabu hiki ni wa aina mbali mbali. Baadhi nawakumbuka vizuri, kama vile Mhashamu Askofu Owdenburg Mdegella wa dayosisi ya Iringa ya Kanisa la Kiluteri Tanzania, ambaye alisema kuwa kitabu kimemfurahisha sana na anataka wageni wakisome ili watuelewe wa-Tanzania. Aliniambia hayo siku tulipokutana kwenye chuo cha Peace House, Arusha, na alikuwa anaongea kutokana na uzoefu wake mkubwa wa kuwapokea na kushughulika na wa-Marekani wanaokuja Tanzania katika mpango wa ushirikiano baina ya waumini wa-Marekani na wa-Tanzania uitwao Bega kwa Bega.

Mwingine ninayemkumbuka vizuri ni Balozi Mstaafu Andrew Daraja. Alikisoma kitabu hiki wakati akiwa balozi wa Tanzania hapa Marekani, na alinipigia simu akaniambia jinsi alivyokipenda kitabu hiki kama nyenzo ya kuweka maelewano baina wa wa-Marekani na sisi wa-Afrika.

Mzee Patrick Hemingway, katika maongezi naye, amekuwa akikisifia kitabu hiki. Siku tulipomtembelea, alisema kuwa kitabu hiki ni "tool of survival." Mzee huyu m-Marekani anajua anachokisema, kwani aliishi Tanganyika (baadaye Tanzania) kwa miaka yapata 25. Ninaguswa na maoni ya watu kama yeye, ambao wanajua hali halisi ya tofauti baina ya utamaduni wao na wetu.

Katika miaka hii kumi, nimepata mialiko kadha wa kadha kutoka kwenye vyuo, taasisi, makampuni, na vikundi, kwenda kutoa mihadhara kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake. Ingawa kitabu hiki ni kifupi tu kilichoandikwa kwa lugha rahisi, wala si cha kitaaluma, kimenisaidia kuendesha mihadhara hiyo na pia warsha, na hata kutatua migogoro ya kutoelewana baina ya wa-Marekani na wahamiaji na wakimbizi kutoka Afrika.

Ninawashukuru kwa namna ya pekee watu waliochangia kwa namna moja au nyingine kwa kukisoma kitabu, kuwaelezea wengine, na kunipa maoni yao. Wiki hii nitawakumbuka kwa namna ya pekee.

Mambo ni mengi sana yaliyotokea katika miaka hii kumi, ambayo ningeweza kuyaandikia kitabu. Panapo majaliwa, nitafanya hivyo.

Friday, May 23, 2014

Tunawazia Kwenda Tena Montana Kuonana na Mzee Patrick Hemingway

Mwishoni mwa mwezi Aprili, mwaka jana nilienda Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway. Huyu ni mzee wa miaka 86 sasa, na ndiye mtoto pekee aliyebaki wa mwandishi maarufu, Ernest Hemingway. Niliandika kifupi kuhusu safari hii katika blogu hii.

Tulisafiri watu watano. Wanafunzi wangu ambao wanaonekana kushoto kabisa pichani, baba ya huyu mwanafunzi aliyevaa kaptura, na rubani wa ndege ya huyu baba mzazi. Mzazi wa mwanafunzi na rubani wake hawamo pichani. Mzee anayeonekana pichani ndiye Mzee Patrick Hemingway. Hapa tuko nje ya nyumba yake iliyoko katika mji mdogo wa Craig. Maskani yake hasa hasa, kwa miaka mingi, ni katika mji wa Bozeman, Montana.

Wanafunzi hao wawili ni kati ya wanafunzi 29 wa chuo cha St. Olaf, ambao nilienda nao Tanzania mwezi Januari, 2013, kuwasomesha kuhusu maandishi na safari za Hemingway katika Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54.

Wakati tukiwa Tanzania, wanafunzi hao walinisikia nikiongelea habari za Mzee Patrick Hemingway, kwamba ni mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway, na kwamba nina mawasiliano naye kwa simu, na kwamba ninapangia kwenda Montana kuonana naye.

Huyu mwanafunzi aliyevaa kaptura alisema bila kusita kuwa baba yake angewezeza kutupeleka Montana kwa ndege yake. Hatimaye, siku tuliyopanga, alikuja na ndege yake hapa Minnesota, akitokea nyumbani kwake Ohio. Tulipokutana, nilikuja kufahamu kuwa baba huyu sio tu shabiki wa maandishi ya Hemingway, lakini pia ni msomaji hodari wa vitabu, vya fasihi ya ki-Ingereza, ingawa shughuli zake kimaisha ni biashara.

Kama nilivyogusia kabla, Mzee Patrick Hemingway aliwahi kuishi Tanzania kwa miaka yapata 25 akifanya shughuli kadhaa, ikiwemo ya utalii na kufundisha chuo cha Mweka. Alitukaribisha vizuri sana, tukaongea naye kwa masaa mengi. Huyu mwanafunzi mwingine ni mpiga picha na video, na alirekodi mazungumzo hayo, ambayo ni hazina kubwa. Yana mengi kuhusu maisha, maandishi na mitazamo ya Hemingway, na pia habari nyingi kuhusu waandishi wengine wa nyakati za Hemingway, hasa wale waliokuwa na mawasiliano au uhusiano na Hemingway.

Tuliwazia kwenda tena Montana huu mwezi Mei, kama mwaka jana, lakini kutokana na mimi kuumwa tangu mwanzo wa mwaka, hatujaweza kufanya hiyo safari. Tuna matumaini ya kwenda baada ya miezi michache kuanzia sasa, nitakapokuwa nimepona kabisa, Mungu akipenda.

Kuna mengi bado ya kuongea na Mzee Patrick Hemingway. Jambo moja muhimu ni maisha yake Tanzania. Hilo ni suala ambalo napenda kulifuatilia sana, hasa nikizingatia kuwa mwaka 1954, Hemingway mwenyewe alikwenda hadi Iringa kumtembelea mwanao Patrick akakaa yapat5a wiki tatu. Hiyo ni habari ambayo nataka kuifuatilia kwa undani. Hatujui, huenda Hemingway aliandika hiki au kile kuhusu Iringa, kwani hakuwa mtu aliyekaa mahali asiandike mambo ya mahali hapo. Suala hili linahitaji kufanyiwa utafiti wa kina katika hifadhi ya maandishi ya Hemingway yaliyoiko Cuba na pia maktaba ya John F. Kennedy kule Boston. Mungu akinijalia uzima, nategeme4a kwenda huko miaka ya usoni.

Friday, May 3, 2013

Chakula cha Jioni na Mzee Patrick Hemingway

Kwa siku mbili tatu hivi, nimeandika kuhusu ziara yangu Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliye bado hai wa mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Kwa mfano, soma hapa.

Nilienda na wanafunzi wawili, ambao walikuwa miongoni mwa wanafunzi niliowapeleka Tanzania mwezi Januari mwaka huu, kwa kozi niliyoiita "Hemingway in East Africa." Katika  msafara wetu, alikuwepo pia baba mzazi wa mwanafunzi mmojawapo, ambaye alitupa usafiri wa ndege yake, na rubani wake.

Katika picha hapa kushoto, tunaonekana wote, na mwenyeji wetu, Mzee Patrick Hemingway na mkewe Carol, wakati wa chakula cha jioni. Kutoka kulia kwenda kushoto hapo mezani ni mwanafunzi Jimmy, Mzee Patrick Hemingway, Bwana Cooper (mwenye ndege), rubani, mwanafunzi Clay, Mama Carol, na mimi.

Tulienda kupata chakula cha jioni siku tuliyowasili Montana, yaani tarehe 27. Ilikuwa ni baada ya masaa kadhaa ya kuongea na Mzee Patrick Hemingway, akajibu masuali yangu kuhusu baba yake Ernest Hemingway na maandishi yake yahusuyo Afrika. Hiyo ndiyo ilikuwa sababu ya mimi kuandaa safari hii ya kwenda kumwona.

Mazungumzo yetu yalikuwa marefu, na ilifikia wakati niliona nihitimishe, ili kutomchosha sana Mzee wetu. Lakini Mzee Hemingway ni mwongeaji sana. Pamoja na uzee wake, ana kumbukumbu nzuri sana ya mambo na anapenda kusimulia michapo ya miaka ile ya zamani, ikiwemo ile inayomhususu Ernest Hemingway.

Ziara yetu ilikuwa ya mafanikio makubwa sana. Sote tunakubaliana hivyo, akiwemo Mzee Patrick Hemingway mwenyewe, kama alivyonieleza leo kwenye simu. Leo nimepata barua kutoka kwa mzee mwenye ndege, na kati ya mambo aliyoandika ni "It was a truly remarkable, memorable, and thought provoking weekend."

Tuesday, April 30, 2013

Safari ya Montana Kumwona Mzee Patrick Hemingway

Juzi nilileta ujumbe kuwa nimepata fursa ya kuonana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliye bado hai wa mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Kwangu kama mtafiti na mwalimu, tukio hili ni la kukumbukwa daima. Hapa napenda tu kuongelea mipango ya safari ilivyokuwa.

Nilipokuwa Tanzania mwezi Januari na wanafunzi nikiwafundisha kozi kuhusu Ernest Hemingway, niliwaambia wanafunzi kuwa mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway nina mawasiliano naye kwa simu, na kwamba ni mzee wa miaka 85. Niliwaambia pia kuwa ninapangia kwenda kuonana naye. Mwanafunzi mmoja ambaye amekuwa akirekodi kozi yangu na habari zinazohusika alisema atapenda tutanguzane kwenye hiyo safari. Mwanafunzi mwingine alisema kuwa ana hakika kuwa baba yake atatupeleka kwa ndege yake.

Baada ya kurejea Marekani, tuliendelea na mipango yetu. Niliwasiliana kwa karibu na Mzee Hemingway na huyu kijana wa mwenye ndege aliwasiliana na baba yake, tukakubaliana tufanye safari tarehe 27 wikiendi iliyopita.

Mzee mwenye ndege alikuja kutoka kwao Ohio na rubani wake, nasi tukajumuika nao katika uwanja mdogo wa Lakeville, inavyoonekana pichani kushoto. Kulia kabisa ni mzee mwenye ndege. Kijana wake ni huyu aliyevaa kaptula. Kijana huyu na huyu mwenzake mrefu kabisa ndio wale walifika Tanzania kwenye kozi yangu.

Mzee huyu ni msomi na msomaji wa vitabu. Ni msomaji makini wa mwandishi Hemingway. Wakati nilipokuwa nafundisha kozi yangu kule Tanzania, alitafuta silabasi kutoka chuoni kwangu akafuatilia kozi nzima.

Mzee Hemingway alikuwa ametushauri tukatue uwanja wa Great Falls, Montana. Safari ilichukua yapata masaa matatu, baada ya kutua kwenye mji wa Bismarck, Dakota ya Kaskazini, kwa ajili ya kupata mafuta ya ndege. Hali ya hewa ilikuwa nzuri njia nzima.

Baada ya kufika Great Falls, tulichukua gari tukaenda kwenye mji mdogo wa Craig, ambako Mzee Hemingway alisema angekuwepo.
Tulipata msisimko mkubwa tulipomwona anatungoja nje ya nyumba yake. Nilimwomba hapo hapo tupige picha, kabla hatujaingia ndani kwa mazungumzo, ambayo nitaelezea baadaye. Nimeandika ujumbe huu kwa lengo la kujitunzia kumbukumbu. Mengine ya msingi, yale tuliyojifunza kutoka kwa Mzee Hemingway, yatakuja siku za usoni.

Sunday, April 28, 2013

Hatimaye, Nimeonana na Mzee Patrick Hemingway

Nimerejea jioni kutoka Montana, ambako nilikwenda jana, kuonana na Mzee Patrick Hemingway, mtu maarufu sana. Ni yeye pekee ndiye bado hai kati ya watoto wa mwandishi maarufu Ernest Hemingway.

Mwandishi Hemingway, ambaye alizaliwa mwaka 1899 jirani na Chicago na kufariki 1961, ni maarufu duniani kote. Kwa miaka yapata kumi, nimevutiwa na jinsi alivyoandika kuhusu Afrika, kutokana na kutembelea na kuishi Afrika Mashariki, mwaka 1933-34, na mwaka 1953-54. Ninasoma na kufundisha maandishi ya Hemingway, kama nilivyoandika hapa, na hapa.

Kwa muda mrefu nilitaka niwasiliane na Mzee Patrick Hemingway, ambaye ni mtoto pekee wa Hemingway aliyebaki. Nilifahamu kuwa aliishi Tanzania miaka yapata 25. Moja ya shughuli alizofanya ni kufundisha katika chuo cha Mweka. Nilisoma sana maandishi yake na kusikiliza mazungumzo yake ambayo yako mtandaoni.

Nilijua kuwa huyu ni hazina kubwa kwa yeyote anayefuatilia maandishi na maisha ya Ernest Hemingway. Siku moja, miaka yapata miwili iliyopita, nilijipa moyo nikampigia simu. Nilifurahi jinsi alivyonifanyia ukarimu, tukaongea sana. Kuanzia hapo, nimeongea naye mara kwa mara.

Hatimaye, jana nilisafiri hadi Montana, ambako tumepata fursa ya kuongea kwa masaa mengi, jana na leo. Nimefurahi kwa namna ambayo siwezi hata kuelezea. Nategemea kuandika taarifa mbali mbali za ziara hii siku zijazo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...