Showing posts with label wanafunzi. Show all posts
Showing posts with label wanafunzi. Show all posts

Sunday, December 17, 2017

Tumetoka Darasani

Picha hii ilipigwa tarehe 29 Novemba. Niko na wanafunzi wangu, tukiwa tumetoka darasani. katika somo la "First Year Writing." Hili ni somo la uandishi bora wa ki-Ingereza. Ninalipenda somo hili kama ninavyoyapenda masomo yangu mengine. Darasa letu lina wanafunzi 19.

Baada ya kumaliza kipindi tulitawanyika, lakini dakika chache baadaye nilikutana na hao wawili katika jengo la Buntrock Commons karibu na maktaba, tukapiga picha. Huyu wa katikati anatoka Norway, na huyu mwenzake ni wa hapa Marekani.

Nina bahati na ninafurahi kuwa mwalimu, kushughulika na wanafunzi na vitabu muda wote. Ni kazi ambayo niliitamani tangu nilipokuwa kijana mdogo. Nilipofundishwa ualimu katika chuo kikuu cha Dar es Salaam, ambapo nilisomea Literature, English, na Education, nilifundishwa kuwa mwalimu anashika nafasi ya wazazi, in loco parentis, kwa ki-Latini. Ninawaona wanafunzi kama watoto wangu.

Ninachukulia jukumu langu la kuwaelimisha na kuwalea wanafunzi kwa dhati. Tangu nilipoanza kufundisha, chuo kikuu cha Dar es Salaam, mwaka 1973, nimezingatia wajibu na maadili ya ualimu, ambayo ni kujielimisha kwa bidii, kufundisha kwa uwezo wangu wote, na kuwatendea haki wnafunzi wote bila upendeleo.

Ninafurahi kufundisha hapa chuoni St. Olaf. Walimu wanachapa kazi na uongozi wa chuo unawaheshimu. Wanafunzi wanajua wajibu wao. Wana heshima, na ni wasikivu, wenye dukuduku ya kuhoji na kujua mambo. Ninawapenda. Pamoja na kuwafundisha kwa moyo wote, ninapenda kuwatania. Popote tunapokutana, tunafurahi kama inavyoonekana pichani.

Wednesday, October 25, 2017

Ninangojea Mwaliko Kuelezea Tamaduni

Nimeona tangazo la chuo kimoja cha hapa Minnesota kwamba wanajiandaa kuwapeleka wanafunzi kwenye nchi moja ya Afrika. Ni programu ambayo wamekuwa nayo kwa miaka kadhaa. Kila mara, wamekuwa wakitumia kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika maandalizi hayo, ili kufahamu mambo ya msingi ya tofauti za tamaduni. Wamekuwa wakinialika kuongea nao kabla ya safari.

Nilivyoona tangazo nilijisemea kuwa hawa watu lazima watatafuta kitabu changu tena, na watanitafuta tena, kutokana na nilivyoona siku zilizopita. Nimejifunza tangu zamani kuwa unapotoa huduma kwa mteja, toa huduma bora kiasi cha kumfanya mteja asiwe na sababu ya kutafuta huduma kwingine.

Kwa upande wangu, nilijenga uhusiano huu na wateja kwa awamu. Mwanzoni, nilikuwa ninatoa ushauri tu, hasa katika program za kupeleka wanafunzi Afrika, zinazoendeshwa na vyuo mbali mbali vya Marekani. Baadaye, nilichapisha kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences,  na hicho kikawa kinawavutia wateja wapya. Si kwamba kitabu hiki kina kila kitu. Vile vile, wanaonialika hawanialiki nikawasomee hiki kitabu. Wanakuwa wameshakisoma, ila wanakuwa na shauku ya kujua zaidi kutoka kwangu mwandishi. Kitabu ni kama chambo na kianzio cha mazungumzo.

Ninaandaa kitabu kingine cha kuendeleza yaliyomo katika Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitakuwa na mwelekeo ule ule na mtindo ule ule, ila kitaibua mambo mapya. Tayari nimeshakipa jina, Chickens in the Bus, ambacho ni kichwa cha sura mojawapo katika kitabu hiki.

Friday, June 2, 2017

Kitabu Kimependekezwa na Africa International University

Nimeona leo kuwa kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimependekezwa na Africa International University (AIU) kwa ajili ya wanafunzi wa kigeni. Chuo hiki kiko Karen, nchini Kenya.

Nimevutiwa na maelezo yaliyotolewa kama Information for International Students juu ya hali halisi anayokumbana nayo mtu anapojikuta katika utamaduni wa kigeni:

Moving to a different cultural environment is a very stressful experience – that’s why it is sometimes referred to as “culture shock”. You will likely go through a difficult period of adjustment and homesickness after the initial excitement wears off. This is normal. As you learn your way around the campus and its unique culture, you will be more comfortable at AIU. Soon you will be helping other new international students adjust to AIU and Kenya. If you are willing to learn, you will learn a great deal about yourself and others who are different from you. You will leave here enriched and transformed.

Still, it is wise to take time before coming to prepare yourself and your family for the cultural adjustments that will be necessary. By reading as much as you can about cultural adjustment and talking to other international students, you can learn what to expect. Then you will better understand the feelings and frustrations you deal with as you adjust to your new environment. Since academics will demand a great deal of you at AIU, any preparation you can do before coming will help all of your adjustments once you arrive on campus....Due to cultural differences, you may feel somewhat confused when talking with fellow students. “What do they mean?” Communication in Africa is inferential rather than direct, so you will need to become adept at listening for what is being communicated between the lines.... Students at AIU are coming from all over Africa and the world. They will appreciate the time you invest in learning about the uniqueness of their own cultures—e.g. what communicates respect.

Maelezo na mawaidha haya yanahusiana na yaliyomo katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ni masuala yasiyokwepeka, hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Yanawahusu sio tu wanafunzi, bali pia wafanya biashara, wanadiplomasia, na kadhalika, kama ninavyoelezea mara kwa mara katika blogu hii.

Wednesday, September 29, 2010

Programu za Kupeleka Wanafunzi Tanzania

Leo hapa chuoni St. Olaf tulikuwa na shughuli ya kuzitangaza programu za masomo ambamo chuo kinapeleka wanafunzi wake.

Tunafanya hivyo mara moja kwa mwaka. Walimu washauri wa programu tunakuwepo na taarifa mbali mbali za programu tunazohusika nazo, na wanafunzi wanakuja kupata taarifa hizo, na pia kujiandikisha iwapo wana nia ya kujiunga na programu hizo.

Vyuo vingi hapa Marekani vina programu za aina hiyo, na vyuo kadhaa vinapeleka wanafunzi Tanzania. Hii inatokana na kufahamu faida wanayopata wanafunzi kwa kwenda kuishi na kujifunza katika nchi zingine. Inapanua akili na upeo. Kuishi miongoni mwa watu wa utamaduni tofauti kunampa kijana fursa ya kukomaa kwa namna mbali mbali na kuwa tayari kwa maisha ya zama zetu za utandawazi wa leo. Programu hizi zinachangia maelewano mema duniani.

Pamoja kazi yangu ya kufundisha katika idara ya ki-Ingereza hapa St. Olaf, ninashughulika katika program zinazopeleka wanafunzi nchi za ki-Afrika, ikiwemo Tanzania. Nimefanya shughuli hii kwa miaka yote niliyofundisha hapa ughaibuni, katika programu kama LCCT, ACM Tanzania, na ACM Botswana. Leo nilijipanga kwenye meza kama inavyoonekana katika picha, nikingojea wanafunzi, nimwage sera.

Hii ni fursa ya kuitangaza nchi. Kama nilivyowahi kusema kwenye blogu hii, picha ni vielelezo murua kabisa. Ni lazima niseme kuwa shughuli hii ya kuitangaza Tanzania ilikuwa inanipendeza sana miaka ya mwanzo, wakati Tanzania ilipokuwa kweli nchi ya kupigiwa mfano, ambayo nilikuwa najivunia. Tanzania ile, ya Mwalimu Nyerere, inatoweka. Nchi inazidi kuwa ya matabaka ya wenye mali wanaostarehe, na maskini wanaoteseka. Badala ya jamii yenye amani na utulivu, tunaendelea kuona kushamiri kwa ukatili kama ule unaofanywa dhidi ya albino na wale wanaoitwa vibaka. Program hizi za kuleta wanafunzi Tanzania zinaiingizia nchi hela nyingi, lakini naogopa kuwa hela hizi zinachotwa na mafisadi. Siku hizi, ninapowaambia wanafunzi hao kwenda Tanzania, ninasema nikiwa na wasi wasi. Lakini naendelea kufanya shughuli hii, kwani ni muhimu, sio tu kwa hao wanafunzi, bali kwa nchi yetu na yao, na dunia kwa ujumla, kama nilivyoandika hapa.

Saturday, August 14, 2010

Nimefika Lutheran Junior Seminary, Morogoro

Juzi nilienda Lutheran Junior Seminary, Morogoro, kuangalia kitengo cha ufundishaji wa ki-Swahili na Utamaduni.

Kwa miaka mingi nilifahamu habari za kitengo hiki, kupitia mtandao wao, ila sikuwahi kuwatembelea. Nilifurahi kuonana na walimu na kutembezwa katika mazingira ya shule.


Kwa vile ninashughulika na program za kuleta wanafunzi wa Marekani hapa Tanzania na kwingineko Afrika, niliona ni muhimu nipate ufahamu mzuri wa kitengo hiki cha Morogoro, endapo tutahitaji kuwaleta wanafunzi wetu.

Nilitambulishwa kwa mwalimu ambaye alikuwa darasani akiwafundisha wageni somo la utamaduni. Kumbe anakifahamu kitabu changu cha Africans and Americans na anakitumia. Nilifurahi kuona kuwa niliyoandika yanawanufaisha wengi, hadi huku Morogoro.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...