Showing posts with label The Sun Also Rises. Show all posts
Showing posts with label The Sun Also Rises. Show all posts

Monday, January 30, 2017

Kitabu Nilichonunua Leo: "The Highly Paid Expert"

Leo nilikwenda Minneapolis na wakati wa kurudi, nilipita Mall of America, kuangalia vitabu katika duka la Barnes & Noble. Nilitaka hasa kuona kama kuna vitabu vipya juu ya mwandishi Ernest Hemingway.

Niliangalia scheme vinapowekwa vitabu vya fasihi, nikakuta kitabu kipya juu ya Ernest Hemingway, Everybody Behaves Badly: The Backstory to 'The Sun Also Rises.' kilichoandikwa na Lesley M.M. Blume. Kwa kuwa nimezama sana katika uandishi wa Hemingway, maisha na falsafa yake, na kwa kuwa nimeshasoma The Sun Also Rises, nilitamani kukinunua kitabu hiki, ambacho, kwa maelezo niliyoyaona, kinazungumzia yaliyo nyuma ya pazia.

Sikuwa na hela za kutosha, kwa hivyo nikaamua kuangalia vitabu vingine. Nilitumia muda zaidi katika sehemu ya "Business/Management." Huwa ninapenda sana kununua na kusoma vitabu vya taaluma hii, kwani vinanifundisha mengi kuhusu mambo ya ujasiriamali na biashara. Taaluma hii inanisaidia katika kuendesha shughuli za kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants.

Hatimaye, nilikiona kitabu kilichonivutia kwa namna ya pekee, The Highly Paid Expert, kilichoandikwa na Debbie Allen.  Kwa mujibu maelezo nyuma ya kitabu, huyu mwandishi ni mtaalam maarufu katika mambo ya biashara na ujasiriamali. Niliangalia ndani, nikaona mada anazoongelea ni za kuelimisha kabisa, kama vile matumizi ya tekinolojia za mawasiliano na mitandao.

Niliona anatoa ushauri wa kusisimua. Kwa mfano, anasema kuwa ni lazima mtu unayetaka mafanikio katika shughuli zako, uwasaidie wengine kufanikiwa. Unavyowasaidia wengine wafanikiwe, unajijengea mtandao wenye manufaa kwako pia. Ubinafsi na uchoyo wa maarifa haukuletei mafanikio. Kitabu hiki kinavutia kwa jinsi mwandishi anavyothibitisha mawazo yake, ambayo kijuu juu yanaonekana kama ya mtu anayeota ndoto.

Kwa bahati niliweza kuimudu gharama ya kitabu hiki, nikakinunua na kuondoka zangu, kwani nilikuwa sina hela iliyosalia. Sijutii kununua vitabu. Vitabu vinavyoelimisha ni mtaji, kwani hakuna mtaji muhimu zaidi ya elimu. Kwa wajasiriamali, wafanya biashara, watoa huduma, na kwa kila mtu, elimu ni tegemeo na nguzo muhimu. Ulazima wa kununua vitabu ni sawa na ilivyo lazima kwa mkulima kununua pembejeo.

Saturday, June 25, 2016

Ninasoma "A Moveable Feast"

Nina tabia ya kusoma vitu vingi bila mpangilio, na niliwahi kutamka hivyo katika blogu hii. Kwa siku, naweza kusoma kurasa kadhaa za kitabu fulani, kurasa kadhaa za kitabu kingine, makala hii au ile, na kadhalika. Sina nidhamu, na sijui kama kuna umuhimu wa kuwa na nidhamu katika usomaji.

Siku kadhaa zilizopita, niliandika katika blogu hii kuhusu vitabu nilivyochukua katika safari yangu ya Boston. Nilisema kuwa kitabu kimojawapo kilikuwa A Moveable Feast cha Ernest Hemingway. Ni kweli, nilikuwa ninakisoma, sambamba na vitabu vingine, makala na kadhalika. Matokeo yake ni kuwa inachukua muda kumaliza kitabu.

A Moveable Feast ni kitabu kimojawapo maarufu sana cha Hemingway. Wako wahahiki wanaokiona kuwa kitabu bora kuliko vingine vya Hemingway, ingawa wengine wanataja vitabu tofauti, kama vile A Farewell to Arms, For Whom the Bell Tolls, na The Old Man and the Sea. Hemingway alikuwa mwandishi bora kiasi kwamba kila msomaji anaona chaguo lake.

Ninavyosoma A Moveable Feast, ninaguswa na umahiri wa Hemingway wa kuelezea mambo, kuanzia tabia za binadamu hadi mandhari za mahali mbali mbali. Picha ninayopata ya mji wa Paris na maisha ya watu katika mji huo miaka ya elfu moja mia tisa na ishirini na kitu haiwezi kusahaulika. Ni tofauti na picha ya Paris tuliyo nayo leo.

Hemingway haongelei maisha ya starehe na ulimbwende. Watu wanaishi maisha ya kawaida, na wengine, kama yeye mwenyewe na mke wake Hadley, wanaishi maisha ya shida. Mara kwa mara Hemingway anaongelea alivyokuwa na shida ya hela, ikambidi hata mara moja moja kuacha kula ili kuokoa hela.

Inasikitisha kusikia habari kama hizi, lakini pamoja na shida zake, Hemingway anasisitiza kwamba Paris ulikuwa mji bora kwa mwandishi kuishi. Anasema kuwa gharama za maisha hazikuwa kubwa. Alikuwa na fursa ya kuwa na waandishi maarufu waliomsaidia kukua katika uandishi, kama vile Gertrude Stein, Ezra Pound, na Scott Fitzgerald.

A Moveable Feast, kama vile Green Hills of Africa, ni kitabu chenye kuongelea sana uandishi na waandishi. Hemingway anatueleza alivyokuwa anasoma, akitegemea fursa zilizokuwepo, kama vile duka la vitabu la Shakespeare and Company lililomilikiwa na Sylvia Beach. Anatuambia alivyowasoma waandishi kama Turgenev, Tolstoy, D.H. Lawrence, na Anton Chekhov. Anatueleza alivyokuwa anajadiliana na wengine kuhusu waandishi hao.

Hayo, kama nilivyogusia, yananikumbusha Green Hills of Africa, ambamo kuna mengi kuhusu uandishi na waandishi. Katika Green Hills of Africa, tunamsikia Hemingway akiongelea uandishi hasa katika mazungumzo yake na mhusika aitwaye Koritchner. Vitabu kama A Moveable Feast vinatajirisha akili ya msomaji. Si vitabu vya msimu, bali ni urithi wa kudumu kwa wanadamu tangu zamani vilipoandikwa hadi miaka ya usoni.

Toleo la A Moveable Feast ninalosoma ni jipya ambalo limeandaliwa na Sean Hemingway. Toleo la mwanzo liliandaliwa na Mary Welsh Hemingway, mke wa nne wa Hemingway. Kutokana na taarifa mbali mbali, ninafahamu kuwa kuna tofauti fulani baina ya matoleo haya mawili, hasa kuhusu Pauline, mke wa pili wa Hemingway. Sean Hemingway amerejesha maandishi ya Hemingway juu ya Pauline ambayo Mary hakuyaweka katika toleo lake. Bahati nzuri ni kuwa miswada ya kitabu chochote cha Hemingway imehifadhiwa, kama nilivyojionea katika maktaba ya JF Kennedy.

Jambo moja linalonivutia katika maandishi ya Hemingway ni jinsi anavyorudia baadhi ya mambo kutoka andiko moja hadi jingine, iwe ni kitabu au hadithi, insha au barua. Kwa namna hiyo, tunapata mwanga fulani juu ya mambo yaliyokuwa muhimu mawazoni mwa Hemingway. Mfano moja ni namna Hemingway anavyoelezea athari mbaya za fedha katika uandishi. Mwandishi anaposukumwa au kuvutwa na fedha au mategemeo ya fedha anaporomoka kiuandishi. Dhana hiyo ya Hemingway inanikumbusha waliyosema Karl Marx na Friedrich Engels katika The Communist Manifesto, yakaongelewa pia na wengine waliofuata mwelekeo wa ki-Marxisti, kama vile Vladimir Ilyich Lenin.


Monday, April 6, 2015

Bemidji Yamwenzi Mary, Mke wa Hemingway

Jioni ya tarehe 4 Aprili, baada ya kurejea kutoka Leech Lake Tribal College karibu na mji wa Bemidji, niliingia mtandaoni nikiwa na lengo la kuona kama kuna taarifa zozote kuhusu mkutano wetu. Katika ukurasa wa Facebook wa Chuo, niliona taarifa na picha za mkutano ule:

Hilo lilinivutia. Lakini niliona pia taarifa nyingine, kuhusu namna mji wa Bemidji unavyomwenzi Mary Welsh, aliyekuwa mke wa nne na wa mwisho wa Ernest Hemingway. Mary Welsh alizaliwa karibu na Bemidji akakulia na kusoma mjini hapo.

Kisha alienda kusoma katika Chuo Kikuu cha Northwestern karibu na Chicago. Alikuja kuwa mwandishi katika magazeti hapo Chicago na hatimaye London, akajipambanua kama mwandishi wa habari za vita. Huko ndiko alikokutana na Ernest Hemingway na baadaye wakafunga ndoa.

Nilifahamu hayo yote na mengine mengi, kutokana na utafiti wangu wa miaka kadhaa. Nilifahamu tangu zamani kuwa Mary Welsh alizaliwa eneo la Bemidji, na nilikuwa nawazia kwenda kule kufanya utafiti juu yake. Mary Welsh Hemingway alitanguzana na Ernest Hemingway katika safari ya Afrika Mashariki mwaka 1953-54. Walizunguka Kenya, Tanganyika, hadi Uganda, ambako walipata ajali mbili za ndege, mfululizo.

Mary Hemingway alisafiri hadi Mbeya, na ameelezea hayo na mengi mengine katika kitabu chake kiitwacho How it Was. Nasikitika kuwa wa-Tanzania, kwa kukosa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu, hawafahamu hayo. Wangekuwa wana utamaduni huo, wangeweza kutumia habari na maandishi kama haya ya Mary Welsh Hemingway na Hemingway mwenyewe kwa manufaa makubwa, hasa katika utalii. Hali ni mbaya kwamba wa-Tanzania hawashtuki wakielezwa habari za vitabu namna hii. Nimethibitisha hayo, kama nilivyoandika katika blogu hii.

Wenzetu katika nchi kama Cuba, Hispania na Marekani wanafaidika sana na maandishi ya Hemingway. Cuba wanaitunza sana nyumba ya Hemingway, Finca Vigia, na hata baa alimokuwa anakunywa, mjini Havana, ni kivutio kikubwa cha watalii. Kule Hispania kuna mji wa Pamplona ambao ulipata umaarufu duniani na umaarufu huu unaendelea, baada ya Hemingway kuutembelea na kuangalia mchezo wa "bull fighting," akaandika juu yake katika riwaya iitwayo The Sun Also Rises. Maelfu ya watalii wanafurika Pamplona. Hapa Marekani, nyumba alimoishi Hemingway, kama vile kule Oak Park (Illinois)na Key West (Florida), ni vivutio vikubwa kwa watalii.

Hayo ndio yaliyonijia akilini wakati nasoma taarifa ya mji wa Bemidji kumwenzi Mary Welsh Hemingway. Jambo moja kubwa lililoelezwa katika taarifa ile ni utunzi wa tamthilia juu ya Mary Welsh Hemingway, unaofanywa na Catie Belleveau baada ya utafiti wa muda mrefu.

Hoja sio kwamba ni lazima nasi tujitose na kujishughulisha na Hemingway na mke wake, ingawa kufanya hivyo kungetuletea manufaa kama wanayopata wenzetu wa Cuba, Pamplona, Oak Park na Key West. Ninachotaka kusisitiza ni umuhimu wa kujifunza kutoka kwa hao wenzetu.

Sisi tunao waandishi maarufu kama Mgeni bin Faqihi wa Bagamoyo, aliyetunga Utenzi wa Ras il Ghuli. Je, tunajua habari zake? Tunaye Shaaban Robert. Je, ni wa-Tanzania wangapi wanajua angalau mahali alipozaliwa, sehemu alimoishi, na mahali alipozikwa? Je? wahusika katika wizara za utalii na utamaduni wanafahamu habari hizo? Na je, wanafahamu kuwa taarifa hizo ni hazina ambayo tungeweza kuitumi? Binafsi ninatekeleza wajibu wangu kwa kuandika kuhusu mambo haya, kama nilivyofanya katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, ambacho nitashangaa kikipata wasomaji Tanzania.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...